ASKOFU PENGO: CHUO CHA MTAKATIFU JOSEPH (SJUIT) HAKIMLAZIMISHI MTU KUFUATA MISINGI YA KIKATOLIKI

Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo amewataka watu wasiogope kwenda au kuwapeleka wengine kusoma katika Chuo cha Mtakatifu Joseph (SJUIT) kwa kuogopa watalazimishwa kufuata imani ya chuo hicho kinachoongozwa kwa misingi ya dini ya kikatoliki.

Askofu Pengo amesema hayo jana Ijumaa Machi 8, katika mkutano wa kulitangaza Baraza jipya la chuo lililotangazwa na Mkuu wa Chuo hicho uliofanyika jijini Dar es Salaam.


Alisema licha ya chuo kuwa na malengo ya kikatoliki ambayo yana dini ndani yake na kuna maeneo ambayo lazima yatabaki hivyo, haimaanishi kila mwanafunzi anapaswa kubadili na kuwa mkatoliki.


“Mimi nikija katika chuo hiki ntaingia kama Askofu na kama mkatoliki ambaye ninaamini Yesu ni mwana wa Mungu, lakini hii haimaanishi kila anayekuja kusoma hapa lazima afate misimamo yangu, kila mtu ana imani tofauti na ana haki ya kuwa na imani tofauti.


“Jambo la msingi ni kuwa na misimamo ya kidini ambayo inaongoza maisha ya binadamu, na nitaendelea kusisitiza kuwa kila binadamu aliumbwa na Mungu na maelekezo na maadili yote yanafundishwa kuhusu Mungu mmoja, haijalishi ni dhehebu gani ila tunapaswa kujua Mungu huja kabla ya kila kitu,” alisema Askofu Pengo.


Awali akisoma majina ya baraza hilo jipya Mkuu wa Chuo hicho, Padri Arul Raj aliwataka wajumbe wateule kufanya kazi zao kwa umakini wa hali ya juu ili kukisaidia chuo kutoa elimu itakayozalisha wanafunzi bora ambao wataisaidia nchi kukua katika nyanja mbalimbali hasa ya viwanda ili kuendana na sera ya serikali ya ‘Tanzania ya Viwanda’.


“Lengo la mwanzilishi wa chuo hiki ni kutoa wanafunzi wenye taaluma za Sayansi na Teknolojia, hivyo sisi tumepewa dhamana ya kuhakikisha jambo hili linatimia, hivyo basi inatupasa kuweka nguvu na akili zetu katika kuzalisha wanafunzi watakao isaidia nchi ya Tanzania kukua hasa katika sekta ya viwanda na uhandisi,”alisema.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527