MTOTO WA RUGE AMUOMBEA MSAMAHA BABA YAKE KWA ALIOWAKOSEA ENZI ZA UHAI WAKE

 Mwachi ambaye ni mtoto wa kwanza wa marehemu, Ruge Mutahaba amemuombea msamaha baba yake kwa watu aliowakosea enzi za uhai wake.

Mwachi aliyasema hayo leo Jumamosi Machi 2, 2019 wakati akisoma wasifu wa baba yake katika shughuli za kumuaga zinazoendelea katika viwanja ya Karimjee jijini Dar es Salaam.

“Ninamuombea msamaha baba yangu kwa wale wote aliowakosea enzi za uhai wake, nasi tunawasamehe wote waliomkosea baba,” amesema Mwachi ambaye ni mmoja kati ya watoto watano wa marehemu huku kauli hiyo ikizidisha simanzi kwa waombolezaji

Amesema baba yake alikuwa mtu aliyejitoa kwa wengine mpaka familia ilifikia wakati inaona watu wa nje wanamfaidi kuliko wao.

“Alitenga muda mwingi kusaidia kwa kuzingatia misingi ya utu, alipambana kwa hali zote kufanikisha mambo mengi katika jamii,” alisema huku akijitahidi kujizuia kutoa machozi.

Amesema jamii inachoweza kufanya ni kuchukua jukumu la kusaidia japo Watanzania wawili, watafanikisha ndoto za wengi.
Na Asna Kaniki na Tumain Msowoya, Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527