MBOWE AMTAKA MBUNGE WA CHADEMA ALIYENG'OLEWA UBUNGE AELEZE KILICHOTOKEA

 Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe amemwagiza aliyekuwa mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari kuzungumza kile kilichotokea hadi kuvuliwa ubunge.

Mbowe ametoa agizo hilo leo Ijumaa Machi 15, 2019 jijini Dar es Salaam alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.

Agizo hilo la Mbowe ambaye ni Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni amelitoa baada ya jana Alhamisi, Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai kuiandikia barua Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) akiitaarifu juu ya Nassari kupoteza sifa za kuwa mbunge kutokana na kutohudhuria mikutano mitatu ya Bunge.

Mbowe amesema halengi kumtetea Nassari lakini amemwagiza kuzungumza na wananchi wa jimbo lake na wanachama juu ya kipi kimetokea.

“Nimezungumza na Nassari jana na hata leo na nikamwambia azungumze na wananchi awaeleze kipi kimetokea kwa sababu mimi ninaamini kuwa Nassari kahudhuria vikao vya Bunge na aende akawaeleze,” amesema Mbowe

“Atazungumza yeye (Nassari), ataeleza kinagaubaga nini kimetokea hata kama Spika na timu yake wataendelea kufanya hayo, kufukuza wabunge...” ameongeza Mbowe.
Na Hellen Hartley, Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527