KUSAGA ASEMA RUGE ALISEMA " SIKU NIKIFA MSILIE,MSHEREHEKEE YALE MAZURI NILIYOFANYA"

Mkurugenzi Mtendaji wa Clouds Media Group, Joseph Kusaga, ameeleza kuwa alikutana na Ruge miaka 25 iliyopita wakati akifanya kazi za disko na wakati huo Ruge akiwa mwanafunzi nchini Marekani ambapo walianzisha urafiki kisha kukaa pamoja na kutengeneza wazo la kuanzisha redio.

Kusaga amesema hayo leo Jumamosi, Machi 2, 2019 katika Viwanja vya Karimjee wakati akitoa wasifu wa marehemu Ruge kabla ya kuagwa mwili wake.

“Ruge alipokuja miaka 25 iliyopita, biashara ya kupiga muziki ilikuwa uhuni..tuliiitwa wahuni…..wimbo wa kwanza kutengeneza pale Mawingu uliitwa ‘Oya Msela oooyaaa’… Tulipopeleka kwenye redio tukaambiwa mnaona sasa wahuni hawa, wimbo gani unaitwa Msela?

“Ruge alitengeneza kina Ruge wengine wengi ambao wapo Clouds, na mimi binafsi kupitia Foundation itakayokuja hivi karibuni nitahakikisha tunaendeleza yale aliyokuwa akifanya Ruge Mutahaba,” alisema Kusaga.

Akielezea kwa utulivu wa majonzi miongoni mwa mambo aliyoambiwa na marehemu, Kusaga alisema kwamba Ruge alimwambia: “Siku nikifa, msilie, msherehekee, msifie yale mazuri mtakayoona niliyafanya…”

Kusaga alisema kwamba maneno hayo alimwambia wakati alipokwenda kumwona nchini India wakati wa matibabu yake ambapo alikwenda kwa kushtukiza na ambapo wawili hao walikumbatiana bila kujua kwamba ilikuwa ni mara yao ya mwisho kufanya hivyo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527