WIMBI LA WATOTO KUBAKWA NA WATU WASIOJULIKANA LAIBUKA MBEYA

Wananchi wa Mamlaka ya Mji Mdogo wa Mbalizi katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, wameingiwa na hofu baada ya kuibuka wimbi la ubakaji wa watoto unaotekelezwa na watu wasiojulikana huku vitendo hivyo vikihusishwa na imani za kishirikina.

Wameeleza hofu ya kuibuka kwa wimbi hilo kwenye mkutano wa hadhara ambao umefanyika katika Kitongoji cha Mapinduzi na kuhudhuriwa na makundi mbalimbali wakiwemo viongozi wa dini, viongozi wa mila, watetezi wa Haki za binaadamu na Jeshi la Polisi.

Mwenyekiti wa Kitongoji cha Mapinduzi, Tukubagha Mnyanya, amesema matukio hayo yalianza kusikika Februari 14 mwaka huu ambapo binti wa darasa la saba alibakwa na watu wasiojulikana wakati anatoka shuleni jioni.

Mchungaji wa Kanisa la Evangelistic Assemblies of God Tanzania (EAGT), Vumilia Mwasenga, ameeleza kuwa watoto wengine watatu walivyonusulika kubakwa jumapili wakiwa kanisani.

Diwani wa Kata hiyo, Kisman Mwangomale amesema katika Kitongoji cha Mapinduzi matukio ya ajabu yamekuwa yakitokea sana kwa madai kuwa kuna watu wamekuwa wakiuawa na kufichwa ndani.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527