BUNGE LAAHIRISHWA DODOMA,WAZIRI MKUU ASEMA MAUAJI NJOMBE YANAFANYWA NA WAHUNI WACHACHE


Waziri Mkuu wa Tanzania, Kasimu Majaliwa leo Jumamosi Februari 9,2019 ametoa hoja ya kuahirisha mkutano wa 14 wa Bunge la 11 jijini Dodoma huku akitoa maagizo kwa watendaji.


Kabla ya kutoa hoja hiyo, Majaliwa amewataka viongozi wa mikoa, wilaya na vijiji kukutana na viongozi wa dini kujadiliana masuala ya maendeleo.

Amesema mkutano uliofanyika kati ya viongozi wa dini na Rais John Magufuli ulikuwa na tija hivyo ni muhimu viongozi wakaiga mfano huo.

Amebainisha kuwa mkutano wa Rais Magufuli na viongozi wa dini ulionyesha viongozi hao wana mchango mkubwa ambao hautakiwi kubezwa.

Kiongozi huyo amegusia mauaji ya watoto mkoani Njombe akisema yanafanywa na wahuni wachache.

Majaliwa amesema kauli ya Serikali iliyosomwa bungeni na Waziri wa Mambo ya Ndani, Kangi Lugola ilionyesha hadi sasa watoto saba wameripotiwa kuuawa na mmoja kujeruhiwa.

“Lakini tayari watuhumiwa zaidi ya 29 wamekamatwa kwa uchunguzi," amesema Majaliwa

Waziri Mkuu amesema Serikali inalaani vitendo vyote vibaya vinavyofanywa dhidi ya watoto.


Na Habel Chidawali, Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527