MAPYA YAIBUKA KISA CHA MTOTO ALIYEFUNGIWA KABATINI

Neema Matimbe (15) akiwa na mwanaye.

Uongozi wa hospitali ya Mkoa wa Dodoma umesema kuwa tayari wamemruhusu, Neema Matimbe (15) ambaye inadaiwa mwanaye wa miezi mitano alifungiwa kabatini na mwajiri wake tangu alipozaliwa, lakini hajapata mtu wa kumchukua hivyo atakaa hospitali wakati uongozi ukiwasiliana na
Idara ya Ustawi wa Jamii ili waishi nae kwa sasa.

Imebainika kuwa mama mzazi wa Neema (15) naye ni mfanyakazi wa ndani kama alivyo mwanaye, hivyo kutokana na sababu hiyo, hospitali hiyo imesema ni vigumu kumruhusu binti huyo kwa sababu ya usalama wake.

Akizungumza na www.eatv.tv leo Januari 15, mganga mfawidhi wa hospitali hiyo, Ernest Ibenzi amesema mama wa binti huyo yupo lakini naye anafanya kazi za ndani jijini Dodoma, jambo ambalo ni ngumu kwa binti huyo kuruhusiwa kuishi naye.

Mwalimu Anitha Kimako anayedaiwa kuwa mwajiri wa binti huyo ambaye anatuhumiwa kumpiga na kumshinikiza kumuweka mwanaye kabatini tangu alipozaliwa, alifikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Dodoma Januari 7 na kusomewa shtaka la kushambulia mwili ambalo alilikana na kesi hiyo kuahirishwa hadi Februari 7.

Wakati hayo yakiendelea, kijana anayedaiwa kumpa ujauzito binti huyo na kumkataa, Salum Waziri atafikishwa mahakamani muda wowote kujibu mashtaka ya kumpa mimba mtoto aliye chini ya umri wa miaka 18.

Chanzo:Eatv

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527