CAG AMJIBU SPIKA NDUGAI...ASEMA ANA NIA YA KUHOJIWA

Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu Hesabu za Serikali (CAG), Profesa Mussa Assad amesema ana nia ya kuitikia wito wa Spika Job Ndugai kwa sababu ofisi yake haiwezi kufikia ufanisi unaohitajika katika utendaji wake kama ripoti zake hazifanyiwi kazi ya kuridhisha na Bunge.

Profesa Assad ametoa kauli hiyo leo Alhamisi Januari 17, 2019 katika mkutano wake na waandishi wa habari huku akibainisha kuwa neno udhaifu ni la kawaida kwa wakaguzi katika kutoa maoni ya utendaji wa mifumo ya taasisi mbalimbali.

Mkaguzi mkuu huyo wa hesabu za Serikali ametoa kauli hiyo baada ya kuibuka mzozo kati yake na Ndugai kutokana na Profesa Assad wakati akihojiwa na Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa kusema kushindwa kutekelezwa kwa ripoti anazowasilisha bungeni huenda kunatokana na udhaifu wa chombo hicho kauli ambayo Ndugai alisema ni ya kudhalilisha Bunge na kumtaka kufika mbele ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge Januari 21, 2019 kuhojiwa.

Amesema majibu yake yaliyozua mjadala hayakuwa na nia ya kuidhalilisha Bunge kama dhaifu bali ni lugha ya kawaida kwa wakaguzi katika kutoa maoni ya utendaji wa mfumo wa taasisi mbalimbali.

" Ni wazi kuwa watu wengine wanaweza kuchukua tafsiri tofauti ya maneno kama haya. Yametokea malumbano makali na marefu katika nyanja zote za mawasiliano kuhusu rai, nafasi na maamuzi mbalimbali yaliyochukuliwa na viongozi,” amesema Assad.

“Binafsi na ofisi ya Taifa ya ukaguzi hatuna namna ya kuathiri tafsiri za viongozi, wanasiasa na wachangiaji wa kawaida. Tunachoshauriana ni uungwana utawala katika mawasiliano.”

Na Bakari Kiango, Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527