MIZENGO PINDA AELEZA ALIVYOUMIZWA NA WAPINZANI...NAYE KUUTAKA URAIS

Waziri Mkuu mstaafu, Mizengo Pinda ameweka wazi jinsi alivyokuwa akiumizwa na kauli za upinzani dhidi ya uongozi wake.

Akifungua Baraza la Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM), Mkoa wa Dodoma jana, Pinda alisema kuna kipindi wakati wa uongozi wake, wapinzani walikuwa wakiinyooshea kidole Serikali yao kuwa ni dhaifu haina makali, hivyo walikuwa wanataka kiongozi mkali na mwenye uamuzi mgumu.

Alisema alikuwa haipendi kauli hiyo na ilikuwa ikimkera kwa sababu ilimlenga na yeye, lakini akasema sasa anashangaa kuona wapinzani haohao wameanza kulalamika tena juu ya utendaji kazi wa Rais John Magufuli ambaye ndiye kiongozi wa aina waliyekuwa wakitamani kumpata.

Pinda aliteuliwa kuwa waziri mkuu na Rais wa Awamu ya Nne, Jakaya Kikwete baada ya Edward Lowassa kujiuzulu.

Mwaka 2015, alikuwa miongoni mwa wanachama wa CCM waliojitokeza kugombea urais lakini jina lake liliondolewa katika hatua za awali.

Jana, mstaafu huyo alitumia jukwaa la UVCCM kutoa yaliyo moyoni mwake ikiwa ni miaka mitatu ya tangu Rais Magufuli aingie madarakani mwaka 2015.

Alisema Rais Magufuli ndiye kiongozi ambaye Watanzania walikuwa wanamhitaji kutokana na uthubutu alionao katika kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo.

“Wakati ule kauli hii ilikuwa inaniudhi kwa sababu ilikuwa inanilenga mimi lakini sasa hivi tena ambapo Mungu amesikia kilio chao na kuwapa JPM wameanza kulalamika tena, ni jambo la kushangaza,” alisema Pinda.

“Wakati fulani kuna baadhi ya watu huwa wananiuliza, hivi mzee na wewe si ulikuwa unautaka urais, nawajibu tu aka huyuhuyu ndiye anayefaa, mimi ni miongoni mwa watu wanaomkubali sana Magufuli.”

Alisema Rais Magufuli ametekeleza miradi iliyoanzishwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere ambayo serikali nyingine zilishindwa kuitekeleza kwa kisingizio cha kuogopa gharama kubwa.


Na Rachel Chibwete, Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527