WATUMISHI WAMKERA WAZIRI MKUU...KESHO KUKUTANA NA MAWAZIRI NA MAKATIBU WOTE

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amekagua ujenzi wa eneo la Mji wa Serikali lililoko Ihumwa na kubaini kuwa baadhi ya wakandarasi hawaendi na kasi inayotarajiwa na Serikali.

Waziri Mkuu ameamua kuitisha kikao cha Mawaziri wote na makatibu wakuu wote kesho (Ijumaa) saa 5 asubuhi ili waeleze kazi hiyo itakamilishwa lini.

Ametoa agizo kauli hiyo leo mchana (Alhamisi, Desemba 27, 2018) mara baada ya kukagua ujenzi wa ofisi za wizara zote pamoja na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali katika eneo la Mtumba lililoko km. 17 kutoka jijini Dodoma.

“Nimekagua maeneo yote na kukuta baadhi ya wakandarasi wanatakiwa kujenga majengo ya wizara nne hadi tano. Sijaridhika na baadhi ya kazi, nimeitisha kikao cha Mawaziri wote kesho ili tuangalie ni mkandarasi yupi anaweza kumudu hii kazi.”

“Nimebaini kuna tatizo kubwa la upatikanaji wa vifaa vya ujenzi kama kokoto, nondo, matofali na kikao cha kesho kitahusisha Mawaziri, Makatibu Wakuu, viongozi wa Mkoa na Jiji la Dodoma, wakandarasi wote ili tukubaliane kazi hii inaisha lini,” amesema.

Akitoa mfano, Waziri Mkuu amesema wajasiriamali wanaotengeza matofali Dodoma wako wengi lakini matofali tyao yako chini ya kiwango, kwa hiyo wanatakiwa watu wa kutengeneza matofali mengi yenye uimara. “Tuna ujenzi wa wizara 24, tunataka matofali imara siyo yale ambayo ukilishika tu, mchanga unamomonyoka,” amesisitiza.

Akisisitiza uharaka wa kazi hiyo, Waziri Mkuu amesema kazi hiyo ina malengo maalum na inatakiwa ikamilike haraka sana. “Tarehe ya mwisho ya kukamilisha ujenzi iliyotolewa na Mheshimiwa Rais ilikuwa Desemba 31, mwaka huu lakini kuna sababu zimetajwa kukwamisha ujenzi huo zikiwemo mvua na uhaba wa kokoto,” amesema.

Hata hivyo, Waziri Mkuu amesifia kazi nzuri iliyofanywa kwenye Ofisi ya Mwanasheria Mkuu, Utumishi, Ujenzi, Katiba na Sheria, Maji na Elimu. Kazi hizo zimefanywa na wakandarasi ambao ni Magereza, SUMA JKT, Wakala wa Majengo (TBA) na Vikosi vya Ujenzi vya Mwanza na Dar es Salaam vilivyoko chini ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

Wakandarasi walioboronga ni JWTZ – Mzinga, National Housing na Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST).

Waziri Mkuu amemwagiza Katibu wa Kamati ya Kitaifa ya kuratibu zoezi la Serikali kuhamia Dodoma, Bw. Meshack Bandawe ahakakishe anapokea taarifa kutoka kila taasisi inayohusika na ujenzi huko Ihumwa na akishaijumuisha, aiwasilishe kwake ifikapo leo jioni.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amemuagiza Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma, Bw. Godwin Kunambi ashirikiane na Mkurugenzi wenzake wa Chamwiono kuhakikisha vijana wengi wanapata fursa za ajira kwenye mradi huo.

“Mkurugenzi wa Jiji wasiliana na Mkurugenzi mwenzako wa Chamwino mhakikishe vijana na akina mama wanakuja kufanya kazi hapa. Pia itisha kikao cha^ waandishi wa habari uwaeleze wananchi wako fursa zilizopo, kuanzia ufyatuaji wa matofali, uuzaji wa nondo, kokoto na utengenezaji wa pavement blocks, hizi zote ni fursa, tuna wizara 24 na mahitaji ni makubwa,” alisisitiza.

Mapema, akitoa taarifa mbele ya Waziri Mkuu, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Vijana), Bw. Anthony Mavunde alisema zoezi la kusafisha eneo la ujenzi wa mji wa Serikali lilianza Novemba 28, mwaka huu.

Alisema wizara zote zimepata viwanja na zimeanza ujenzi isipokuwa Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Vijana) ambao bado wanasubiri kupatiwa fedha.

Alisema kazi ya ujenzi wa Mji wa Serikali inasimamiwa na Kamati ya Kitaifa ya kuratibu zoezi la Serikali kuhamia Dodoma, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa na Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma.

(mwisho)

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527