AGPAHI YAFANIKISHA KUPIMA VVU WATU 800,123 MWANZA, 17,815 WAMEANZISHIWA ARVs


Kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa AGPAHI, Dkt. Sekela Mwakyusa akimkabidhi zawadi Mkuu wa mkoa wa Mwanza,Mheshimiwa John Mongella kutokana na ushirikiano anaotoa kwa AGPAHI kutokomeza VVU na UKIMWI mkoani Mwanza.

Asasi ya Ariel Glaser Pediatric AIDS Health Initiative (AGPAHI) inayolenga kutokomeza UKIMWI kwa watoto na familia  Tanzania imefanikiwa kupima Virusi vya UKIMWI watu 800,123 mkoani Mwanza ambapo kati yao 22,968 wameonekana kuwa na maambukizi na tayari kati yao 17,815 sawa na 78% wameanzishiwa huduma ya ARVs.

Akitoa taarifa katika kikao cha wadau wa afya na ustawi wa jamii mkoa wa Mwanza Novemba 5,2018 jijini Mwanza, Mkurugenzi Mtendaji wa AGPAHI, Dkt. Sekela Mwakyusa alisema takwimu hizo ni za kuanzia mwezi Oktoba 2017 hadi Septemba mwaka 2018.

Alisema katika kipindi hicho pia akina mama wajawazito 113,101 mkoani humo walipimwa VVU ambapo 1,400 walionekana kuambukizwa VVU na kati yao (WAVIU wamama) 1,352 sawa na 97% walianzishiwa dawa za kufubaza makali ya VVU.

Hali hiyo ilichangia watoto 1,912 sawa na asilimia 97 waliozaliwa na akina mama hao, kuzaliwa bila maambukizi.

Aliongeza kuwa mkoani Mwanza wanatoa huduma kwenye vituo 177 vya kutolea huduma na kuwaomba wananchi kuendelea kujitokeza kupima afya zao kujua ili endapo wameathirika waanze ARVs mapema. 

Akizungumzia mikoa yote kwa ujumla ambayo AGPAHI ilikuwa ikifanya kazi zake hadi Septemba 2018 (Shinyanga, Simiyu, Mwanza, Mara, Geita na Tanga) alisema hadi Juni 2018 watu 239,170 walikuwa wakipata huduma za VVU na UKIMWI.

“Hadi Juni 2018, katika mikoa hii, watoto 22,383 waliozaliwa na mama wenye VVU walizaliwa bila maambukizi. 

Pia alisema wanawake 54,248 walifanyiwa uchunguzi wa saratani ya mlango wa kizazi ambapo 2,910 waligunduliwa kuwa na dalili za awali ya saratani ya mlango wa kizazi na kutibiwa.

Kwa upande wake, Mkuu wa mkoa wa Mwanza, Mheshimiwa John Mongella alisema serikali inatambua kazi nzuri zinazofanywa na mashirika na asasi mbalimbali mkoani humo katika mapambano dhidi ya VVU na UKIMWI ili kuhakikisha kuwa maambukizi ya VVU yanatokomezwa katika mkoa huo.

"Nawashukuru sana AGPAHI, mmekuwa wadau muhimu mkoani Mwanza, kwa namna ya pekee kabisa nawashukuru kwa kufadhili kikao hiki cha wadau wa afya ambacho tulishindwa kukifanya kutokana na ufinyu wa bajeti lakini mmejitolea kukiandaa," alieleza Mongella.

ANGALIA PICHA HAPA CHINI
Mkurugenzi Mtendaji wa AGPAHI, Dkt. Sekela Mwakyusa akiwasilisha mada kuhusu kazi zinazofanywa na AGPAHI mkoani Mwanza wakati wa kikao cha wadau wa afya na ustawi wa jamii mkoani humo kilichofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Gold Crest jijini Mwanza Novemba 5,2018.
Mkurugenzi Mtendaji wa AGPAHI, Dkt. Sekela Mwakyusa akizungumza wakati wa kikao cha wadau wa afya na ustawi wa jamii mkoa wa Mwanza.
Mkurugenzi Mtendaji wa AGPAHI, Dkt. Sekela Mwakyusa akiendelea kutoa mada ukumbini.
Mkuu wa mkoa wa Mwanza,Mheshimiwa John Mongella akizungumza wakati wa kikao cha wadau wa afya na ustawi wa jamii mkoa wa Mwanza ambapo aliwashukuru wadau wa afya ikiwemo asasi ya AGPAHI kwa kuendelea kushirikiana na serikali katika mapambano dhidi ya VVU na UKIMWI. 
Mkuu wa wilaya ya Nyamagana, Dkt. Philis Nyimbi akizungumza wakati wa kikao cha wadau wa afya na ustawi wa jamii mkoa wa Mwanza .
Mkuu wa mkoa wa Mwanza,Mheshimiwa John Mongella akizungumza wakati wa kikao hicho.
Wadau wa afya wakiwa ukumbini.
Wadau wa afya wakiwa ukumbini.
Wadau wakiwa ukumbini.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527