HII HAPA KAULI YA MO DEWJI BAADA YA KUACHIWA NA WALIOMTEKA...BABA NAYE KAONGEA


 
Mfanyabiashara maarufu nchini Tanzania, Mohammed Dewji 'Mo' anamshukuru Mungu kwa kumrejesha salama.

Mo aliyepatikana alfajiri ya leo Jumamosi Oktoba 20, 2018 amesema hayo kupitia akaunti ya Twitter ya Kampuni ya Mohamed Enterprise Limited (Metl Group).

"Namshukuru mwenyezi Mungu nimerudi salama nyumbani. Nawashukuru Watanzania wenzangu na watu wote kote duniani kwa dua na sala zao."

"Nashukuru mamlaka zote, ikiwemo jeshi la polisi, zilizofanya kazi ya kuhakikisha narudi salama," amesema Mo 

Naye Gullam Dewji Hussein, baba wa mfanyabiashara Mohammed Dewji ‘Mo Dewji’ amesimulia jinsi alivyompata mwanaye aliyetekwa Oktoba 11, 2018 akibainisha kuwa alipigiwa simu leo alfajiri Oktoba 20, 2018 akielezwa kuwa amepatikana.

Akizungumza na MCL Digital, Gullam amesema alijulishwa kuwa mwanaye amepatikana akiwa katika gari ambalo lilitelekezwa katika viwanja vya Gymkhana jijini hapa.

Amesema Mo Dewji baada ya kushushwa katika gari hilo alitembea kutafuta msaada wa simu.

Amebainisha kuwa baada ya kupokea simu hiyo alifika haraka eneo la tukio na kufanikiwa kumuona mwanaye.

“Namshukuru Mungu nimemkuta Mo akiwa salama na haraka nilimpeleka nyumbani lakini tumemkuta ana majeraha kidogo ila jambo la kushukuru ni kwamba yuko hai,” amesema Gullam.

“Tulipofika nyumbani tulianza kufanya mawasiliano na Jeshi la Polisi kwa kuwapa taarifa kuwa kijana wangu nimempata na wao (polisi) walifika nyumbani kwangu Oysterbay.”

Gullam amemshukuru Rais John Magufuli kwa kufanikisha kupatikana kwa mwanaye.
Via >>Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527