POLISI DAR WADAI KUUA MAJAMBAZI WATATU

Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limekamata bastola moja aina ya Browing namba A 183847 ikiwa na risasi tatu ndani ya magazine pamoja na Shotgun iliyotengenezwa kienyeji.


Akithibitisha tukio hilo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari leo, Kamanda wa Polisi Kanda maalumu ya Dar es Salaam Lazaro Mambosasa, amesema tukio hilo lilitokea mnamo Agosti 29, mwaka huu majira ya saa moja jioni katika Bar ya Big Brother iliyopo Mbagala kiburugwa.


” Agosti 29 2018 saa moja jioni huko maeneo ya Baa ya Big Brother iliyopo Mbagala kiburugwa Jeshi la Polisi Kanda maalumu ya Dar es Salaam liliwakurupusha wahalifu katika baa hiyo wanaodhaniwa kuwa walikuwa wanapanga njama za kufanya uhalifu.

“Baada ya wahalifu hao kuwaona askari walianza kujihami kwa kurusha risasi kuwashambulia, askari walijibu mapigo na kufanikiwa kuwajeruhi wahalifu watatu wanaume wanaokadiriwa kuwa na miaka (30-38) na wawili kufanikiwa kukimbia kusikojulikana, walipopekuliwa walikutwa na silaha mbili,”amesema.

Majeruhi walifariki dunia wakati wakipelekwa hospitali, na miili yao imehifadhiwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili(MNH), Jeshi la Polisi linaendelea na msako mkali kuwasaka wahalifu wengine waliokimbia.


Aidha katika tukio jingine Mambosasa amesema Jeshi hilo limefanikiwa kukusanya kodi za tozo za makosa mbalimbali ya usalama barabarani kufikia kiasi cha zaidi ya bilioni 2.3, kiasi hiki kimekusanywa kuanzia Agosti 1 hadi Agosti 30 mwaka huu na kukamata magari 57,716 na Pikipiki 1872.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527