MUSWADA WA BODI YA WALIMU WAWASILISHWA BUNGENI

Serikali imewasilisha bungeni Muswada wa Sheria ya Bodi ya Kitaalamu ya Walimu Tanzania ya Mwaka 2018 itakayokuwa na majukumu mbalimbali yakiwamo ya kuweka viwango vya utaalamu wa ualimu.


Akiwasilisha muswada huo bungeni leo Jumatano Septemba 5, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako amesema madhumuni ya muswada huo ni kuweka muundo wa kisheria wa usimamizi na uendeshaji wa Bodi ya Kitaalamu ya Walimu ambayo pamoja na mambo mengine itakuwa na jukumu la kuinua kiwango cha utaalamu wa ualimu kwa lengo la kuhakikisha walimu wanakuwa na viwango stahiki kitaaluma.


“Serikali inatarajia kwamba baada ya sheria hii kupita na kutekelezwa, matokeo yatakuwa kuinua hadhi ya taaluma ya ualimu na walimu kwa kusajili walimu wote kulingana na viwango vyao vya weledi na kuwapa leseni ya kufundisha katika ngazi stahiki, kulindwa kwa hadhi ya taaluma na utaalamu wa ualimu kwa kuzuia watu wasiokidhi vigezo na viwango stahiki kufanya kazi ya ualimu na mengineyo,” amesema Profesa Ndalichako.


Aidha, amesema hali ilivyo sasa kutokana na idadi kubwa ya walimu, kumekuwapo na changamoto zinazohitaji kuwa na mfumo thabiti wa usimamizi wa ubora wa walimu na taaluma ya ualimu.


“Vile vile, kwa kuzingatia Itifaki ya Soko la Pamoja la Afrika Mashariki, wananchi wa nchi wanachama wana uhuru wa kufanya kazi katika nchi za Jumuiya,” amesema.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527