BABA MTAKATIFU ATUMA SALAMU ZA POLE AJALI YA KIVUKO ILIYOUA WATU ZAIDI YA 130 TANZANIA


Baba Mtakatifu anawaombea waathirika kwa ajili ya ajali ya kivuko cha MV Nyerere katika Ziwa la Victoria nchini Tanzania 
Baba Mtakatifu Francisko ametuma ujumbe kwa raia, viongozi wa Kanisa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kufuatia na ajali ya kivuko iliyotokea Alhamis 20 Septemba 2018 katika ziwa Victoria. Shughuli za uokaji bado zinaendelea.

Sr. Angela Rwezaula – Vatican

Baba Mtakatifu Francisko ametuma ujumbe wake, uliotiwa saini na Kardinali Petro Parolin, Katibu wa Vatican tarehe 21 Septemba 2018 kwa Balozi wa Vatican nchini Tanzania Askofu Marek Solczynsk,ambapo ametuma ujumbe kwa raia, viongozi wa Kanisa, na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kufuatia na ajali ya kivuko iliyotokea, Alhamis 20 Septemba Tanzania.

Baba Mtakatifu Francisko anaelezea masikitiko yake mara baada ya kupata habari ya ajali ya kivuko cha MV Nyerere ambacho kilipinduka katika Ziwa Victoria, ufukweni mwa Kisiwa cha Ukara tarehe 20 Septemba 2018. 

Katika ujumbe huo, Baba Mtakatifu anaonesha kwa masikitiko moyoni na mshikamano kwa wale wote wanaoomboleza kwa ajili ya kupoteza wapendwa wao na kwa wale ambao bado wanahofia kuwakuta bado hai wale ambao hawajapatikana. 

Kwa wote anaomba baraka ya Mungu iwashukie na kuwakumbatia kwa nguvu na faraja kwa wale waliopatwa na mkasa huo. Kadhalika anawatia moyo viongozi wa raia na vikosi vya ukoaji wanaoendelea katika juhudi hiyo ya uokoaji.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527