MKUU WA MKOA AITULIZA FAMILIA YA MWANAFUNZI ALIYEUAWA KWA KIPGO.......MKUU WA SHULE, MAKAMU WAKE NA AFISA ELIMU KATA WASIMAMISHWA KAZI

Kifo cha mwanafunzi wa shule ya msingi Kibeta Siperius Eradius aliyedaiwa kuuawa na mwalimu wake kimeondoka na walimu watatu huku familia ya marehemu ikikubaliana na uchunguzi ambao haujawekwa wazi.


Akizungumza leo Alhamisi Agosti 30, 2018 Mkuu wa Mkoa wa Kagera Brigedia Jenerali Marco Gaguti baada ya kutembelea shule hiyo, amemuagiza mkurugenzi wa manispaa ya Bukoba awasimamishe kazi walimu watatu ili wachunguzwe kama walitekeleza majukumu yao.


Waliosimamishwa ni Renatha Izidory aliyekuwa mwalimu mkuu na msaidizi wake Sunday Elisha na ofisa elimu wa Kata ya Kibeta, Hashimu Mponda.


Mkuu huyo wa mkoa pia amekwenda kwa familia ya marehemu na kubainisha kuwa familia hiyo imekubaliana na matokeo ya uchunguzi wa pili wa kifo cha mwanafunzi huyo uliofanywa na madaktari kutoka nje ya Mkoa wa Kagera.


Awali, familia hiyo ilisusia mwili wa mwanafunzi huyo baada ya uchunguzi uliotolewa na mganga mfawidhi wa Hospitali ya rufaa Mkoa wa Kagera, Dk John Mwombeki kueleza kuwa mwili wake ulikutwa na alama zinazoonyesha alipigwa siku kadhaa kabla ya kukutwa na umauti.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527