MUGABE AKATAA KUMUUNGA MKONO MNANGAGWA


Rais wa zamani wa Zimbabwe, Robert Mugabe (kulia) akiwa na mrithi wake Rais wa sasa Emmerson Mnangagwa.

Rais wa zamani wa Zimbabwe, Robert Mugabe amesema hamuungi mkono mrithi wake Rais wa sasa Emmerson Mnangagwa ndani ya chama tawala Zanu PF, kwa kile alichodai kuondolewa kwa nguvu madarakani na chama alichokianzisha.

Mzee Mugabe mwenye umri wa miaka 94, ametoa kauli hiyo wakati wa mkutano wake na wanahabari Jijini Harare, ikiwa zimesalia saa kadhaa kabla ya taifa hilo la kusini mwa Afrika kufanya uchaguzi mkuu hapo kesho.

Mugabe amesisitiza kuwa, hawezi kuwapigia kura watu waliomtesa na kwamba kura yake atampigia mmoja kati ya wagombea wengine 22 wanaowania nafasi ya urais.

"Namtakia kila kheri kiongozi wa chama cha upinzani cha Vuguvugu la Mageuzi ya Kidemokrasia, MDC, Nelson Chamisa katika uchaguzi wa kesho. Kijana huyu ndio anaonekana kufanya vizuri na ndiye mgombea anayefaa", amesema Mugabe.

Zaidi ya raia milioni tano wa Zimbabwe wanajiandaa kumchagua Rais kwa mara ya kwanza katika kipindi cha miaka 38 bila Mugabe madarakani.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527