MBUNGE WA CHADEMA WAITARA ASEMA UGOMVI WAKE NA MBOWE NDIYO SABABU YA KUHAMIA CCM

Mbunge wa Ukonga, Mwita Waitara amesema kilichosababisha kujivua uanachama wa Chadema na kujiunga na CCM ni Uenyekiti.


Waitara ametangaza uamuzi wa kujiunga na CCM leo Julai 28 katika mkutano na wanahabari uliofanyika Ofisi za CCM, Lumumba.


“Shida ni uenyekiti wa Chadema, ukianzia kwa akina Chacha Wangwe, Zitto Kabwe, hata mimi ni uenyekiti hapo kuna shida,” amesema.


Amesema suala la uenyekiti sio lake peke yake bali wapo wabunge wengi wanaoguswa nalo lakini hataki kuwataja kwa majina.


“Kuna kikao tulikaa na wabunge wengi wa majimbo na viti maalumu tukawa tunazungumza kwamba Tundu Lissu agombee uenyekiti baadaye hoja hiyo wakaicha mimi nikaendelea nayo. Wakaniambia ninataka Tundu Lissu agombee au ni mimi mwenyewe?” amesema na kuongeza:


“Mbowe amewahi kuniambia kamanda unanipinga na mimi ntakushughulikia na kwenye Chadema bado hakuna mtu kama yupo ntamng'oa hikii chama ni mali yangu.”


Waitara amesema kwamba ugomvi huo uliibuka kwa sababu mchakato wa Uchaguzi ndani ya chama hicho unakaribia na kosa lake ni pale alipotaka kujua ni kwa nini kiongozi huyo mpaka sasa anaendelea kushikilia Uenyekiti kwa takribani miaka 20 sasa.

"Sisi watu wa Tarime tulishaathiriwa naCHADEMA, Marehemu Chacha Wangwe alisema kwamba anataka kugombea nafasi y Uenyekit na Mbowe alimuambia kwamba atamshughulikia na sasa hatunaye. Sasa mimi nimeona bora nikimbie kabla sijashughulikiwa" Waitara.

Mbali na hayo Waitara amesema kwa kuwa anatamani kuwatumikia wananchi wa Ukonga amelazimika kuhamia CCM illi aweze kufanya kazi kwa kushirikiana na serikali katika kuwaletea maendeleo wananchi wake.

"Mimi nimeona kabla hawajanipiga chini nijiondoe mwenyewe. Sasa ndani ya CHADEMA, ukionekana na mtu wa CCM unaulizwa kwa nini unaonekana na watu hao. Mimi shida yangu siyo CCM shida yangu ni kuona wananchi wangu wa Ukonga wanatatuliwa shida zao. Wananchi wa Ukonga wavumilie natafuta namna bora ya kuweza kuwana viongozi wa serikali bila kuhojiwa kama nimefumaniwa na mke wa mtu. Nimetaka kuwa huru" ameongeza.

Waitara amesema amejivua uanachama kwa kutumia Katiba ya CHADEMA, Ibara ya 5.41 ambapo ameweka wazi atakuwa siyo Mbunge wa Ukonga na hakihitaji tena chama hicho "Nimetupa jongoo na mti wake".

Waitara amesema uamuazi wake wa kuhamia CCM tayari ameungwa mkono na wazee wa jadi wa Musoma, na watu wake wa karibu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527