AZAM FC NA SIMBA SC WATAVUKA VIKWAZO??


Wachezaji wa Azam FC (kushoto) na Simba (kulia) katika matukio tofauti kwenye moja ya mechi zao kwenye Kombe la Kagame.
***
Klabu za soka za Azam FC na Simba SC zina nafasi ya kuweka rekodi endapo tu zitafanikiwa kushinda mechi zake za nusu fainali ya michuano ya Kombe la Kagame ambazo zinachezwa leo jioni kwenye uwanja wa taifa jijini Dar es salaam.

Mchezo wa nusu fainali ya kwanza kati ya Gor Mahia dhidi ya Azam FC ni kumbukumbu ya fainali ya mwaka 2015 ambayo iliwapatia Azam FC ubingwa wao wa kwanza wa Kombe hilo kwa kushinda mabao 2-0. Baada ya hapo Gor Mahia imekuwa ni timu imara na yenye changamoto kwa timu za Tanzania.

Endapo Azam FC watafanikiwa kushinda leo dhidi ya Gor Mahia, watakuwa wamejiweka kwenye mazingira mazuri ya kutetea ubingwa wao ambao wanaushikilia tangu mwaka 2015. Ikumbukwe kuwa michuano hii haikufanyika katika miaka ya 2016 na 2017.

Kwa upande wa Simba ambao ndio mabingwa wa historia wa kombe hilo, wakiwa wamelitwaa mara sita, wanashuka dimbani kucheza na mabingwa wa Zanzibar JKU. Endapo Simba watafanikiwa kutinga hatua ya fainali watakuwa wanakaribia kuendelea kupanua rekodi yao kwa kutwaa taji la 7.

Katika mechi zao za robo fainali Azam FC ilishinda mabao 4-2 dhidi ya Rayon Sports ya Rwanda huku Simba ikishinda bao 1-0 dhidi ya AS Ports ya Djibouti. JKU wao waliitoa Singida United kwa penati 4-3 huku Gor Mahia wakiifunga 2-1 timu ya Vipers ya Uganda.

Je, Azam na Simba watavuka vikwazo ili mmoja wao akaweke rekodi au Gor Mahia na JKU wataweka maajabu na kutengeneza historia mpya ? Mechi ya kwanza Azam FC na Gor Mahia inaanza saa 8:00 Mchana huku Simba na JKU ikianza saa 11:00 Jioni.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527