Picha : MANISPAA YA SHINYANGA YAENDESHA MDAHALO WA MAADHIMISHO YA SIKU YA MAZINGIRA DUNIANI

Kuelekea Kilele cha Siku ya Mazingira duniani Juni 5,2018,Manispaa ya Shinyanga imeendesha mdahalo wa maadhimisho ya siku ya mazingira duniani kwa kuwakutanisha pamoja maafisa watendaji wa kata 17 za manispaa hiyo kujadili namna ya kutunza mazingira katika manispaa hiyo.


Mdahalo huo ulioongozwa na Mkurugenzi wa halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga,Geofrey Mwangulumbi umefanyika leo Jumamosi Juni 2,2018 katika ukumbi wa mikutano wa manispaa hiyo .

Akifungua mdahalo huo,Mwangulumbi alisema jukumu la kutunza mazingira ni kila mwananchi hivyo kuwataka wananchi kutunza mazingira ili kuepusha mkoa wa Shinyanga kuwa katika hatari ya kuwa jangwa.

Alisema ili kutunza mazingira ni vyema wananchi wakaacha kutumia mkaa unaotokana na miti na badala yake kutumia nishati mbadala ikiwemo matumizi ya mkaa unaotokana na taka mbalimbali kama vile karatasi na mapumba.

Aidha aliwaka maafisa watendaji kusimamia kikamilifu sheria za utunzaji mazingira huku akiwatahadharisha kuepuka kuwapiga faini wananchi bila kuzingatia sheria ikiwemo kutoa risti za EFD zinazokubalika kisheria.

“Ni marufuku kwa mwananchi yeyote kutozwa faini bila kupewa risti halali kwa mujibu wa sheria kwani faini bila risti ni ubadhirifu,nanyi wananchi msikubali kutoa faini bila kupewa risti za kielektroniki ‘EFD”,alieleza Mwangulumbi.

Mkurugenzi huyo wa Manispaa ya Shinyanga aliwahamasisha wananchi kuendelea kupanda miti na kutorohusu mifugo kuzurura ovyo mtaani huku akiwataka viongozi kuendelea kuhamasisha wananchi kupanda miti.

Wadau hao wa mazingira kwa  pamoja walijadili hali ya utunzaji wa mazingira ,mafanikio changamoto na mikakati iliyopo,
maoni na mapendekezo ya wadau kuhusu namna bora ya uhifadhi wa mazingira katika manispaa hiyo.

Mjadala uliongozwa na swali :Nini unadhani kitasaidia kufanikisha kampeni ya serikali ya utunzaji mazingira ikiwemo wananchi kuacha matumizi ya mkaa na badala yake kutumia nishati mbadala ambayo inatajwa kuwa na gharama nafuu kuliko mkaa?.


Kauli mbiu ya taifa ya  maadhimisho ya siku ya Mazingira  duniani mwaka huu ni ‘Mkaa ni gharama tumia nishati mbadala’.

ANGALIA PICHA ZA MATUKIO HAPA CHINI

Mkurugenzi wa halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga,Geofrey Mwangulumbi akifungua mdahalo wa maadhimisho ya siku ya mazingira duniani kwa maafisa watendaji wa kata katika anispaa ya Shinyanga.Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog
Mkurugenzi wa halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga,Geofrey Mwangulumbi akizungumza wakati wa mdahalo huo uliongozwa na swali : Nini unadhani kitasaidia kufanikisha kampeni ya serikali ya utunzaji mazingira ikiwemo wananchi kuacha matumizi ya mkaa na badala yake kutumia nishati mbadala ambayo inatajwa kuwa na gharama nafuu kuliko mkaa?.
Wa kwanza kushoto ni Afisa Nyuki na Misitu kutoka NAFRAC wilaya ya Shinyanga,Franael Sumari akifuatiwa na Mtaalamu wa takataka kutoka Ujerumani Dorothea Kruse na Afisa Mazingira Manispaa ya Shinyanga Ezra Manjerenga
Afisa Mazingira Manispaa ya Shinyanga Ezra Manjerenga akizungumza wakati wa mdahalo huo na kubainisha kuwa hiyo ni sehemu ya maadhimisho ya siku ya mazingira duniani ambapo kilele chake kitakuwa Juni 5,2018.
Afisa Nyuki na Misitu kutoka NAFRAC wilaya ya Shinyanga,Franael Sumari akieleza kuhusu hali ya misitu na ufugaji nyuki katika manispaa ya Shinyanga. Pamoja na mambo mengine alisema ufugaji nyuki unasaidia utunzaji mazingira.
Mtaalamu wa takataka kutoka Ujerumani Dorothea Kruse akifafanua namna ya kutumia taka ngumu kutunza mazingira.
Afisa Mtendaji kata ya Ngokolo Salum Soud akichangia mada wakati wa mdahalo huo.
Afisa Mtendaji kata ya Ibinzamata,Mwajuma Bakari akichangia hoja wakati wa mdahalo huo.
Afisa Mtendaji kata ya Shinyanga Mjini Simon Mashishanga akichangia mada wakati wa mdahalo huo.
Kaimu Afisa Mtendaji kata ya Kitangiri,Ansila Materu akizungumza wakati wa mdahalo huo.
Wadau wa mazingira wakiandika dondoo muhimu wakati wa mdahalo huo.
Maafisa watendaji wa kata ya Shinyanga Mjini na Ibadakuli wakiwa ukumbini.
Katibu wa chama walimu wastaafu Mkoa wa Shinyanga,Nsolo Stephen akielezea namna chama hicho kinavyoshiriki katika shughuli za utunzaji mazingira. Alisema wameanzisha mradi wa kutengeneza mkaa kwa kutumia takataka mbalimbali.
Afisa Mtendaji kata ya Ndala Seleman Katonga akichangia mada wakati wa mdahalo huo
Wadau wa mazingira wakiwa ukumbini.
Mdahalo unaendelea.
Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527