MBOWE AANGUKA GHAFLA...KALAZWA MUHIMBILI


Mahakama imeambiwa kuwa mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amelazwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili baada ya kudondoka ghafla alfajiri.


Jeremiah Mtobesya ambaye ni wakili wa Mbowe, aliiambia Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbard Mashauri, kuwa mteja wake alianguka leo Juni 18,2018 akiwa nyumbani kwake.

Kadhalika, Mahakama imeelezwa kuwa Mbowe ambaye pia ni mbunge wa Hai, amefiwa na kaka yake, Henry Mbowe.

Akiwasilisha taarifa hiyo, Wakili Mtobesya alieleza kuwa Mbowe ambaye ni mshtakiwa namba moja katika kesi namba 112 ya 2018 amefiwa na kaka yake usiku wa kuamkia leo.

Awali Wakili wa Serikali Mkuu, Faraja Nchimbi aliiambia mahakama kuwa kesi ilipangwa kwa ajili ya washtakiwa Mbowe na wenzake wanane kusomewa maelezo ya awali PH na kwamba wamejiandaa na wapo tayari.

Hata hivyo aliiambia mahakama kuwa Juni 12 na 14 , 2018 walipokea mapingamizi ya kisheria na kwamba wapo tayari kuendelea na mapingamizi hayo.

Na Tausi Ally, Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527