HIZI NDIYO MECHI MBILI ZA 16 BORA KOMBE LA DUNIA



Wachezaji wa Morocco na Hispania wakigombea mpira wakati wa mchezo.

Baada ya mechi nne za leo za kufunga makundi ya A na B kwenye Fainali za Kombe la Dunia kumalizika, hatimaye mechi mbili za raundi ya 16 bora zimefahamika ambapo Ureno itacheza na Uruguay huku wenyeji Urusi wakikabiliana na Hispania.

Katika mechi mbili za Kundi B zilizomalizika leo usiku, zimeshuhudiwa zikimalizika kwa sare ambapo Hispania imetoka sare ya 2-2 na Morocco huku Ureno ikitoka sare ya 1-1 na Iran. Hispania itacheza na mshindi wa pili wa Kundi A ambaye ni mwenyeji Urusi na Ureno itacheza na mshindi wa kwanza Uruguay.

Katika mechi ya Ureno dhidi ya Iran zimeshuhudiwa penati mbili ambapo Cristiano Ronaldo alikosa huku Karim Ansarifard akipata kwa upande wa Iran. Penati hizo zimefanya michuano hii kufikisha penati 20 hadi sasa ambayo ni idadi kubwa zaidi kuwahi kutokea katika historia ya Fainali za Kombe la Dunia.

Ureno pia wamefanikiwa kusonga mbele kutoka hatua ya makundi kwa mara ya nne katika historia yao ya kucheza Kombe la Dunia. Wamefanya hivyo katika miaka ya 1966, 2006, 2010 na 2018.

Wachezaji wa Ureno na Iran wakibishana na mwamuzi katika moja ya maamuzi wakati wa mchezo.

Naye mshambuliaji wa Hispania Iago Aspas ambaye amefunga bao la kusawazisha la Hispania, sasa amehusika katika mabao 8 kwenye mechi 8 za Hispania hivi karibuni. Amefunga matano na kusaidia matatu. Hispania pia wamefanikiwa kumaliza hatua ya makundi bila kupoteza mechi tangu wafanye hivyo mwaka 2006.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527