KAKA AMUUA DADA YAKE UGOMVI WA JARUBA..AACHIWA POLISI..DC SHINYANGA AAGIZA AKAMATWE TENA


Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro, ameliagiza Jeshi la Polisi kumkamata kwa mara ya pili  Kanda Lunebula anayetuhumiwa kumuua dada yake Holo Lunebula mkazi wa kijiji cha Ihalo kata ya Ilola Shinyanga vijijini na kisha kuachiwa huru na polisi kutokana na ushahidi usioacha shaka kuhusu mauaji hayo kukosekana.


Matiro alitoa maagizo hayo jana Juni 22,2018 kwenye mkutano wa hadhara katika kijiji cha Ihalo wakati akisikiliza kero za wananchi na kuzitatua ambapo alisema kutokana na mashahidi waliopatikana juu ya kusaidia upelelezi wa kesi ya Mauaji ya Holo Lubenula mtuhumiwa huyo wa mauaji Kanda Lunebula anatakiwa akamatwe tena. 

Inaelezwa kuwa mtuhumiwa huyo alimuua  dada yake 'Holo Lubenula' Mei 6, 2018  vichakani katika kijiji cha Ihalo kata ya Ilola Shinyanga vijijini, ambapo alikamatwa na Jeshi la Polisi mara baada ya kudaiwa yeye ndiye aliyehusika na mauaji ya ndugu yake huyo kutokana na kuwa na ugomvi wa muda mrefu kwa kugombania shamba la kilimo cha mpunga 'jaruba'. 


“Naomba wananchi muwe na ushirikiano kwa vyombo vya dola kwa kutoa ushahidi pale mtuhumiwa anapokamatwa ili apate kushughulikiwa na kufungwa jela, kitendo ambacho kitasaidia kumaliza tatizo la mauaji kwenye kijiji hiki, tofauti na hapo mtaendelea kulilaumu jeshi kuwaachia huru watuhumiwa”,alisema Matiro. 

“Hivyo kutokana na watu kupatikana tayari kwa kutoa ushahidi juu ya kesi hiyo ya mauaji akiwemo na mama yake mzazi kwa kumtuhumu mtoto wake huyo wa kiume kumuua dada yake , naagiza kuanzia sasa mtu huyo akamatwe na kesi yake ianze upya,”aliagiza Matiro. 

Awali akiwasilisha kero za wananchi juu ya mauaji ya watu wasio na hatia kwenye kijiji hicho wakiwemo watoto wadogo, Mama mzazi wa mtuhumiwa wa mauaji ya dada yake Milembe Tungu, alisema yupo tayari kutoa ushahidi kuwa mtoto wake Kanda Lunebula ndiye muuaji. 


Alisema watoto wake hao wawili walikuwa na ugomvi siku nyingi wa shamba la kulima mpunga( jaruba), ambapo pia mtoto huyo wa kiume alikwenda kwa mganga wa kienyeji na kuambiwa kuwa ili apate utajiri lazima amuue mama yake au dada yake na alipotekeleza mauaji hayo alikuwa akiishi kwa msongo wa mawazo tofauti na zamani. 


Naye mmoja wa wananchi wa kijiji hicho, Chuna Kidevu alilitupia lawama Jeshi la polisi kwa kuwatakamata watuhumiwa wa mauaji na kisha kuwaachia huru ambapo wamekuwa wakirudi uraiani kuendeleza mauaji huku wakitamba kuwa mtu mwenye pesa hawezi kufungwa jela. 


Kwa upande wake Mkuu wa kituo cha Polisi Kata ya Didia Wilbert Sichone mahali ambapo mtuhumiwa huyo wa mauaji aliswekwa rumande alisema mtuhumiwa huyo aliachiwa baada ya kukosekana kwa ushahidi ambapo walalamikaji hawakuwa tayari kutoa ushirikiano kwa jeshi hilo na hivyo kumuachia. 

TAZAMA MATUKIO KATIKA PICHA HAPA CHINI
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akizungumza na wananchi wa kijiji cha Ihalo kata ya Ilola Shinyanga na kuwaasa kujenga tabia ya kutoa ushahidi mahakamani pale watuhumiwa wa mauaji wanapo kamatwa ili washughulikiwe kisheria na kufungwa jela na hatimaye kumaliza suala la mauaji kwenye kijiji hicho. Picha na Marco Maduhu - Shinyanga
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akizungumza na wananchi wa kijiji cha Ihalo na kuwataka waache tabia ya kuendekeza kuabudu waganga wa kienyeji ambao wamekuwa wakiwachonganisha na ndugu zao na hatimaye kusabaisha mfarakano na mauaji.
Wananchi wa kijiji cha Ihalo wakiwa kwenye mkutano wa hadhara wakisikiliza utatuzi wa kero zao kutoka kwa mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro.
Mwananchi Milembe Tungu akitoa kero ya mauaji ya watu wasio na hatia na kutoa ushahidi kuwa Mwanae Kanda Lunebula anahusika na mauaji ya dada yake Holo Lunebula na hivyo kuomba vyombo vya dola vimshughulikie na yupo tayari kutoa ushahidi.
Mwananchi Chuna Kidevu akizungumza kero ya Jeshi la Polisi kuwa na tabia ya kuachia watuhumiwa wanaokamatwa kuhusika na mauaji ya watu wasio na hatia na hatimaye kurudi uraiani na kuanza kujigamba kuwa mtu mwenye pesa hawezi kufungwa na kisha kuendelea na tabia yake ya mauaji.
Kamanda wa Sungusungu wa kijiji hicho cha Ihalo Masesa Lutaula akizungumza kwenye mkutano huo wa hadhara na kutoa kilio chake cha kutafutwa na baba mdogo wa mtuhumiwa wa mauaji ya dada yake Kanda Lunebula.
Wananchi wakiendelea na mkutano wa hadhara.
Mkuu wa kituo cha Polisi Didia Wilbert Sichone akizungumza kwenye mkutano huo wa hadhara na kuwataka wananchi kujenga tabia ya kutoa ushahidi wa kutosha kwa jeshi hilo ili watuhumiwa wapate kufungwa jela na siyo kuachiwa huru mara baada ya ushahidi kukosekana.
Mkutano ukiendelea.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Ihalo Mashega Maganga awali akifungua mkutano wa hadhara wa mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro wa kusikiliza Kero za wananchi na kuzitatua.
Katibu tawala wa wilaya ya Shinyanga Boniphace Chambi akiruhusu wananchi kuanza kutoa kero zao kwa mkuu wa wilaya ya Shinyanga ili zisikilizwe na kutafutiwa ufumbuzi.
Diwani wa kata ya Ilola Amos Mshandete akizungumza kwenye mkutano huo wa hadhara na kuwataka wananchi wawe huru kutoa kero zao kwa mkuu huyo wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro.
Mwananchi Felista Jilatu akiomba kutatuliwa kero ya wanachama wa CHF ambapo pale wanapofika kwenye zahanati ya kata hiyo hupewa dawa za Panado tu, na kupewa majibu kuwa tatizo hilo limeshashughulikiwa toka zamani na dawa zipo za kutosha, ikiwa matatizo hayo ya uhaba wa dawa yalikuwa ya kipindi cha nyuma
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akizungumza kwenye mkutano wa hadhara na kuwataka wananchi wajenge tabia ya kushiriki kwenye shughuli za uchangiaji wa maendeleo mbalimbali ikiwamo kumalizia ujenzi wa zahanati katika kijiji hicho cha Ihalo.
Mwananchi Mohamedi Saidi akizungumza kwenye mkutano huo wa hadhara.
Wananchi wa kijiji cha Ihalo wakiwa kwenye mkutano wa hadhara wa mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro wakisikiliza utatuzi wa kero zao ikiwemo masuala ya afya, ardhi na elimu kwa kutaka kuongezewa walimu wa masomo ya Sayansi
Wananchi wakiendelea na mkutano wa hadhara.
Mkutano ukiendelea wa utatuzi wa kero mbalimbali za wananchi wa kijiji cha Ihalo.
Mkutano ukiendelea.
Wananchi wakisikiliza kwa makini utatuzi wa kero zao kutoka kwa mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro.
Mkutano ukiendelea.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akizungumza kwenye mkutano huo na kuwataka wananchi kero nyingine wana uwezo wa kuzitatua wenyewe ikiwemo suala la kuweka meza za soko.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akiwa amemaliza mkutano wake wa kutatua kero mbalimbali za wananchi wa Kijiji cha Ihalo, hapo akiteta jambo na akina mama wa kijiji hicho.

Na Marco Maduhu - Shinyanga

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527