DC GAGUTI AGAWA HATIMILIKI ZA KIMILA KATA YA MUGERA NA KAJANA BUHIGWE

Halmahsuri ya wilaya ya Buhigwe mkoani Kigoma imeanza zoezi la ugawaji wa hati miliki za kimila katika vijiji vya Mugera, Kajana na Katundu katika kata ya Mugera na Kajana katika kaya 1025 hati ambazo zitasaidia kupunguza migogoro ya ardhi katika wilaya na mkoa kwa ujumla.


Akikabidhi hati miliki hizo katika kaya 50 za mfano jana katika kijiji cha Muhegera kata ya Mugera wilayani humo zinazotolewa na mradi wa usimamizi wa maliasili kwa ajili ya kuongeza kipato kwa mwananchi unaotekelezwa na serikali ya Tanzania na Ubelgiji chini ya shirika la ENABEL, kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Kigoma, Mkuu wa wilaya ya Buhigwe Brigedia Jenerali Marco Gaguti alisema katika kesi 10 zinazofika ofisini kwake kati ya hizo nane ni za migogoro ya ardhi na mbili ni za urithi.

Brigedia Jenerali Gaguti alisema mradi huo utasaidia usalama wa wananchi na kupunguza migogoro ya ardhi ambayo ilisababisha baadhi ya wananchi kupoteza maisha na wengine kubaki wakiwa walemavu, kwa kuwa wananchi wakiwa na maeneo yaliyopimwa na wakiwa na umiliki wa kisheria itasaidia sana kesi hizo kupungua na wananchi wataendelea kufanya shughuli zao za maendeleo na kuachana na tabia iliyokuwepo kwa wananchi wengi kuzunguka kwenye mahakama za ardhi na kupeleka kesi za kuibiana maeneo na kuepuka kutumia gharama nyingi kuendesha kesi hizo.

"Nimefurahi sana kwa mradi huu nimeona maeneo mengi niliyopita kukagua zoezi hili lilivyokwenda nimeona wananchi wengi wanauelewa na wanajua umuhimu wa hati miliki nitoe wito kwa viongozi wa serikali za vijiji muendelee kuwahimiza wananchi kuja kufuatilia hati miliki hizi kwakuwa hati hizo nje na kupunguza migogoro ya ardhi itasaidia sana wananchi kutumia hati hizo kuombaea mikopo kwa ajili ya kuendeleza biashara zao", alisema mkuu huyo.

"Wote wanaouelewa faida ya kwanza ni usalama mtu akimiliki hati yake ana uhakika wa kumiliki eneo lake kisheria kesi nyingi zinazopokelewa wilayani kati ya kesi kumi kesi saba ni za migogoro ya ardhi na kesi nyingine ni za mirathi imesababisha kwa kiasi kikubwa watu wengi kupoteza maisha",aliongeza.

Hata hivyo alisema maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya shughuli za msitu wa kupanda mti kuanza zoezi la upandaji miti msimu wa upandaji utakapoanza na kutoa rai kwa viongozi wa vijiji kusimamia ipasavyo maeneo ya huduma za kijamii yaliyopimwa kwa ajili ya shughuli za ufugaji na kilimo yatumike kwa lengo lililokusudia na wananchi waelekezwe namna bora ya kuyatumia na kuepusha migogoro kwa wananchi.

Akitoa taarifa ya mradi mratibu wa mradi huo wilaya ya Buhigwe, William Marandu alisema mpango wa matumizo bora ya ardhi ni tokeo tarajiwa namba mbili la mradi ilipima ukubwa wa ardhi ya Kijiji cha Mugera hekta 9401.856 chenye vitongoji vinne ambavyo ni Ruyange, Mugera, Kishaha na majengo na mradi huo ulianza mwaka 2016 kwa kutenga matumizi ya ardhi ya Maeneo ya kilimo kekari (6117.076) malisho ya mifugo Hekati 1207.1, vyanzo vya maji , maeneo ya maziko , maeneo ya makazi hekari 477.78, misitu ya asili 378 na misitu ya kupandwa hekari 1097.3 kwa kuwa Aridhi ndio chanzo kikubwa cha mtaji wa wananchi.

Alisema hati miliki zilizo gawiwa kwa kaya 50 za mfano ni kati ya hati miliki 1025 zilizoandaliwa na mradi wa (NRMLED) kwa vijiji vitatu vya wilaya ya Buhigwe na hati miliki 975 zilizobaki zitaendelea kutolewa baada ya ufunguzi wa tukio hilo na kutoa wito kwa wananchi wengine ambao bado hawajafanya utaratibu wa kupata hati miliki za kimila kufanya utaratibu waweze kupata hati hizo kwa kupitia Idara ya ardhi ya halmashauri ya wilaya hiyo.

Mmoja kati ya wanufaika wa Mradi wa ugawaji wa hatimiliki za kimila Thadeo Bitumgwa alisema anashukuru kwa kufahamu mipaka ya kiwanja chake ana hakika ya kuwa hatapata mgogoro na mtu yeyote na ana uhakika wa uwarithisha watoto wake eneo ambalo ni salama na bila kuwa na ugomvi na majirani wenzake.

Nae Sospiter Sabuni mkazi wa Mugera alisema hati hiyo anaweza kunufaika nayo kwa shughuli mbalimbali wananchi wengi wamekuwa wakipoteza uhai kwa ajili ya kugombea maeneo, na wengine wamepoteza haki zao za kumiliki kwakuwa hawana hati lakini baada ya kuwa na hati wana uwezo pia wa kupata fidia pindi wanapokuwa maeneo yao yamechukuliwa kwa shughuli zingine za maendeleo kwa kutumia hati hizo wanaweza kupata fidia.

Kwa Mujibu wa Sera ya Taifa ya Ardhi na Sheria za Ardhi Namba nne ya mwaka 1999, sheria ya ardhi ya vijiji Namba tano ya mwaka 1999 , sheria ya mpango ya matumizi bora ya Ardhi Namba sita ya mwaka 2007 kila Kijiji hakina budi kuandaa mpango wa amatumizi bora ya ardhi kwa madhumuni ya kuwezesha usimamizi na matumizi endelevu ya ardhi na maliasili na rasilimali zake zote.

Na Rhoda Ezekiel - Malunde1 blog
ANGALIA PICHA HAPA CHINI
Mkuu wa wilaya ya Buhigwe Brigedia Jenerali Marco Gaguti akionesha hatimiliki kwa wananchi kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Kigoma. Picha zote Rhoda Ezekiel - Malunde1 blog
Mkuu wa wilaya ya Buhigwe Brigedia Jenerali Marco Gaguti akikagawa hatimiliki kwa mwananchi
Mkuu wa wilaya ya Buhigwe Brigedia Jenerali Marco Gaguti akikagawa hatimiliki kwa mwananchi






Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527