SPIKA NDUGAI AMTULIZA MWIJAGE....AMTAKA AKAJIPANGE UPYA AJE NA MAJIBU SAHIHI

Spika wa Bunge Job Ndugai amelazimika kuingilia kati mvutano ulioibuka bungeni kuhusu tofauti ya bei ya sukari kati ya Tanzania Bara na Zanzibar kwa maelezo kuwa majibu yaliyotolewa na Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage juu ya jambo hilo hayajajitosheleza.


Kufuatia sakata hilo, Ndugai amesema swali hilo litaulizwa tena wiki ijayo ili Serikali itoe majibu ya kina, “hili ni swali la msingi sana na linapaswa kutolewa majibu mazuri na Serikali.”


Mvutano huo ulitokana na swali la mbunge wa Mpandae (CCM), Salim Hassan Turky aliyehoji tofauti ya bei hizo na kujibiwa na Mwijage, majibu ambayo mbunge huyo hakuridhika nayo.


Katika maelezo yake Mwijage amesema Tanzania Bara haina uhaba wa sukari na kuwatoa hofu watu mbalimbali.


Kuhusu tofauti ya bei kwa pande mbili za muungano, waziri huyo amesema zaidi ya asilimia 53 ya sukari itumikayo Zanzibar huagizwa kutoka nje kwenye vyanzo ambavyo gharama zake ni nafuu ikilinganishwa na asilimia 29 ya sukari inayoagizwa nje kwa upande wa bara.


Kufuatia majibu hayo Ndugai amesema swali hilo halikujibiwa vyema. Katika swali la msingi Jaku Hashim Ayoub (BLW) alihoji juu ya tofauti ya bei ya bidhaa hiyo katika pande hizo mbili za muungano na kubainisha kuwa gunia la kilo 50 visiwani Zanzibar linauzwa kwa Sh65,000 huku gunia hilo kwa upande wa Tanzania Bara likiuzwa kwa Sh120,000.


Katika majibu yake ya swali la msingi, Mwijage amesema wametoa maagizo kwa viwanda vinne vya kuzalisha sukari nchini kuongeza ulimaji wa miwa katika mashamba yake.


“Bei ya sukari ina maana kubwa kwa maisha ya Watanzania, haiingii akilini bei ya Tanzania Bara kuwa tofauti na ile ya Zanzibar.


"Kama ni kweli wananchi wa Tanzania bara wanalipa sukari mara mbili ya ya Zanznibar ili tu kulinda wenye viwanda....Haiwezekeni hiyo. Bunge linahitaji majibu ya uhakika. " Amesema Spika Ndugai

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527