Picha : MAADHIMISHO YA SIKU YA UHURU WA VYOMBO VYA HABARI MKOA WA SHINYANGA YAFANA


Klabu ya waandishi wa habari mkoani Shinyanga (SPC) leo Alhamis Mei 3,2018 imeungana na waandishi kote duniani kuadhimisha siku ya uhuru wa vyombo vya Habari duniani ambayo hufanyika kila mwaka tarehe 3 Mei. 

Maadhimisho hayo yaliyohudhuriwa na wadau wa habari mkoani Shinyanga yamefanyika katika ukumbi wa Liga Hotel Mjini Shinyanga ambapo mgeni rasmi alikuwa mkuu wa mkoa wa Shinyanga,Mheshimiwa Zainab Telack aliyekuwa ameongozana na kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa.

Kupitia maadhimisho hayo Klabu ya waandishi wa habari mkoani Shinyanga (SPC) imeitaka serikali kutobinya uhuru wa habari ambao ndiyo chachu ya maendedeleo katika nchi ambayo inataka kukua kiuchumi. 

Akizungumza wakati wa maadhimisho hayo, Mwenyekiti wa Klabu ya waandishi wa habari mkoa wa Shinyanga,Kadama Malunde alisema uhuru wa habari ni chachu ya uwajibikaji wa maendeleo katika mkoa ama nchi ambayo inataka kukua kiuchumi na hivyo kuitaka Serikali kutobinya uhuru huo pamoja na kuingia kwenye chuki na waandishi wa habari ambao wamekuwa wakifichua maovu ndani ya jamii na kufikia hatua hata ya kuhatarisha usalama wa maisha yao. 

“Takwimu zinaonesha katika nchi zilizoendelea mwandishi wa Habari anachukuliwa kama nguzo muhimu katika kuibua kero na matatizo mbalimbali yanayoikabili jamii ili yaweze kutatuliwa lakini nchi nyingi katika bara la Afrika, waandishi wa Habari wamekuwa wakichukuliwa kama mahasimu na maadui hali inayosababisha waandishi hao kutokuwa huru hivyo kupunguza ari ya uwajibikaji katika jamii”,alisema Malunde 

"Kutokana na kuwepo kwa tishio hilo la kuminya uhuru wa Habari, tunawasihi waandishi wa Habari ambao kimsingi ni watetezi wa watu wengine kuwa makini na kujilinda ili kuepuka madhara kutoka kwa watu wasiopenda kuona maovu yao yanafichuliwa",alieleza.

"Ili kuwa na taifa lililoendelea, lazima taifa hilo litoe uhuru wa Habari ili waandishi wa Habari wawajibike, hivyo watendaji na wadau wa mkoa wetu wanapaswa kuepuka kubinya uhuru wa habari ili tuweze kufikia maendeleo tuliyoyakusudia ikiwemo hili la uchumi wa viwanda",aliongeza Malunde

Katika hatua nyingine alivitaka vyombo vya ulinzi na usalama, wadau wa maendeleo na viongozi wa kidini na wadau mbalimbali kuunganisha nguvu ya pamoja kupiga vita vitendo vya mauaji ya wanawake kuuawa kwa kukatwa mapanga sababu ya imani za kishirikina. 

Naye mkuu wa mkoa wa Shinyanga Zainabu Telack aliwatoa wasiwasi waandishi hao wa Habari kuwa waendelee kutekeleza majukumu yao kwa nia njema ya kuleta maendeleo kwa nchi katika nyanja zote kwani kila raia ana haki ya kupata taarifa ,kutafuta habari kwa chombo chochote bila ya kuingiliwa. 

Aidha aliwataka waandishi hao pia kujikita kuandika habari ambazo zitakuwa na mguso ndani ya jamii zenye malengo mahususi ya kuhakikisha zinabadilisha maisha yao kutoka hatua moja kwenda nyingine na hatimaye kukua kimaendeleo. 

“Mimi kwenye mkoa wangu nitaendelea kuzifanyia kazi habari zote ambazo zitakuwa zikitolewa na waandishi wa habari kwa kuzitafutia ufumbuzi ili jamii iweze kuisha salama na kufanya shughuli za kiuchumi na hatimaye kukua kimaendeleo,”alisema Telack. 

Kwa upande wake Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani Shinyanga Kamishina msaidizi wa Polisi Simon Haule alipongeza waandishi hao wa habari kwa kushirikiana na jeshi hilo katika kutoa taarifa za uhalifu kupitia vyombo vyao na kuwataka waendelee kufanya kazi zao kwa weledi ili kutokomeza kabisa uhalifu huo na mkoa ubaki kuwa salama. 

Alisema Jeshi hilo litaendelea kuwashughulikia watu wote ambao wataendelea kutenda masuala ya uharifu likiwamo la mauaji hayo ya wanawake yatokanayo na Imani za Kishirikina, kwa kuwatia nguvuni na kuwafikisha mahakamani ili wapate kuchukuliwa hatua kali za kisheria. 

Maadhimisho hayo ya siku ya uhuru wa vyombo vya habari mkoani Shinyanga yaliyokuwa yanarushwa moja moja 'Live' na Radio Faraja Fm Stereo pia yamehudhuriwa na Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya Umoja wa Klabu za Waandishi wa habari nchini - UTPC, Salma Abdul.

Maadhimisho ya siku hii kitaifa yamefanyika jijini Dodoma lakini kwa mujibu wa mwongozo wa wasimamizi wetu UTPC mwaka 2018 kila Klabu imeelekezwa kuadhimisha siku hii kwa ngazi ya mkoa na Kauli mbiu ya klabu zote ni ‘Uhuru wa habari ni chachu ya uwajibikaji wa maendeleo ya mkoa’.

TAZAMA MATUKIO YA PICHA HAPA CHINI
Viongozi wa Klabu ya waandishi wa habari mkoani Shinyanga (SPC) wakiwa na kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa huo ikiongozwa na mwenyekiti wake mkuu wa mkoa huo Zainab Telack wakiwa wamesimama kwa dakika moja kuwakumbuka waandishi wa habari waliofariki dunia - Picha zote na Marco Maduhu - Shinyanga News Blog & Malunde1 blog
Wadau wa habari mkoani Shinyanga nao wakiwa wamesimama kuwakumbuka waandishi wa habari waliofariki dunia.
Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Zainabu Telack akizungumza kwenye maadimisho ya uhuru wa vyombo vya habari mkoani humo na kuahidi serikali kuendelea kushirikiana na vyombo vya habari na kutobinya uhuru wa habari kama katiba yainavyosema kila raia ana uhuru kwa kutafuta na kupata habari bila ya kuingiliwa ili mradi asivunje sheria ya nchi.
Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Zainabu Telack pia aliwataka waandishi hao wa habari kufungua miradi mbalimbali ambayo itakuwa inawaingizia kipato nje ya kazi yao, ili kuondoa changamoto ya kutumika na baadhi ya wadau wenye pesa na hatimaye kuandika habari za uchochezi ambazo zitahatarisha amani ya nchi.
Mwenyekiti wa Klabu ya waandishi wa habari mkoani Shinyanga Kadama Malunde akisoma taarifa kwenye maadimisho hayo ya siku ya uhuru wa vyombo vya habari mkoani humo na kuitaka serikali na wadau wote kuendelea kushirikiana na waandishi wa habari katika kuleta maendeleo na siyo kubinya uhuru wa habari.
Mwenyekiti wa Klabu ya waandishi wa habari mkoani Shinyanga Kadama Malunde pia aliwasisitiza waandishi wa habari kuzingatia maadili ya kazi yao pamoja na kufuata sheria za nchi
Mwenyekiti wa Klabu ya waandishi wa habari mkoani Shinyanga Kadama Malunde aliwasisitiza wadau wa habari pamoja na waandishi wa habari kuwajibika kila mmoja kwa nafasi yake ili kuuletea maendeleo mkoa na nchi kwa ujumla.
Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani Shinyanga Kamishina msaidizi wa Polisi Simon Haule akiwapongeza waandishi wa habari kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kutumia kalamu zao kuelimisha jamii kuachana na masuala ya uhalifu na hatimaye matukio hayo yamepungua kwa kiasi kikubwa likiwemo la mauaji ya vikongwe ambalo halipo kabisa.
Mchungaji Yohana Nzela kutoka kanisa la KKKT Mjini Shinyanga akimwakilisha Askofu wa kanisa hilo Emmanuel Makala, akizungumza ukumbini ambapo aliwataka waandishi wa habari mkoani Shinyanga kujikita pia kuandika habari za watu wanyonge ili kupaza sauti zao waweze kutatuliwa matatizo yao hasa wa maeneo ya vijijini.
Mkuu wa Vikosi vya Jeshi la Wananchi (JWTZ) mkoa wa Shinyanga Kanali Justas Kitta akitoa nasaha kwa waandishi wa habari na kuwataka kuwa wanachuja habari zao kabla ya kuzitoa ili kuepuka kutaharatisha amani ya nchi
Naibu Meya wa Halmashauri ya manispaa ya Shinyanga Agnes Machiya akiwataka waandishi hao wa habari kuunda vikundi vya ujasiriamali au SACCOS ili waweze kwenye kuomba mkopo katika halmashauri hiyo na kuinuka kiuchumi, ili wawe wanaweza kwenda hata vijijini kutafuta habari za wanyonge na kuwapazia sauti, ikiwa wengi wa waandishi hawana mikataba ya ajira na hivyo suala la nauli kwao huwa ni changamoto na hivyo kushindwa kufika maeneo ya pembezoni.
Katibu wa Klabu ya waandishi wa habari mkoani Shinyanga Stephen Wang'anyi akizungumza kwenye maadhimisho hayo ya uhuru wa vyombo vya habari.
Mjumbe wa bodi ya wakurugenzi kutoka (UTPC) Salma Abdul akitoa salamu zake ambapo aliwataka waandishi wa habari wasiwe wepesi wa kukata tamaa pale wanapokumbana na changamoto katika utendaji kazi, ikiwa wao ndiyo sauti kubwa ya wanyonge katika kuwasemea matatizo yao ndani ya serikali.
Mkurugenzi msaidizi wa Radio Faraja iliyopo mjini Shinyanga Anikazi Kumbemba ambaye pia ni Mwandishi Mwandamizi, akielezea historia ya siku ya uhuru wa vyombo vya habari na hali halisi ya uhuru wa vyombo vya habari nchini Tanzania
Mkurugenzi msaidizi wa Radio Faraja iliyopo mjini Shinyanga Anikazi Kumbemba ambaye pia ni Mwandishi Mwandamizi akiwasilisha taarifa yake kwa mkuu wa mkoa wa Shinyanga Zainab Telack
Mdau wa habari Chief Abdalla Sube akichangia mada kwenye maadhimisho hayo ya uhuru wa vyomba vya habari mkoani Shinyanga na kutoa pongezi kwao kwa kuutangaza mkoa wa Shinyanga na kutoa elimu mbalimbali kwa jamii kupitia vyombo vyao vya habari.
Viongozi wa Klabu ya waandishi wa habari mkoani Shinyanga ,wakiwa na kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa huo, meza kuu siku ya maadhimisho ya uhuru wa vyombo vya habari mkoani Shinyanga.
Kamati ya ulinzi na usalama ikiwa kwenye maadhimisho ya uhuru wa vyombo vya habari mkoani Shinyanga.
Mwandishi wa habari kutoka Radio Faraja Faustine Kasala akichangia mada kwenye maadhimisho hayo na kuwataka viongozi pale wanapokuwa wakifanya kazi na waandishi wa habari waache kuwaelekeza namna ya kuandika Habari wanayoitaka, bali wawaachie uhuru ikiwa hiyo ndiyo taaluma yao.
Waandishi wa habari wakiwa kwenye maadhimisho hayo ya uhuru wa vyombo vya habari.
Mwandishi wa habari Shagwe Thani kutoka Radio Free mkono wa Kushoto, akiwa na Nsianel Gelard ambaye ni Ofisa mahusiano ya Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira mjini Shinyanga (SHUWASA), siku ya maadhimisho hayo ya uhuru wa vyombo vya habari mkoani Shinyanga.
Mchungaji David Hamadi kutoka Kanisa la Agape Life Church lililopo Lubaga mjini Shinyanga akiwataka waandishi wa habari kuzingatia maadili yao hasa pale wanapopiga picha na kuzirusha kwenye mitandao ya kijamii.
Kushoto ni mwandishi wa habari wa Radio Free Africa Malaki Philipoakiwa na Moshi Ndugulile mwandishi wa habari Radio Faraja wakiwa ukumbini.
Katibu wa chama cha Walimu manispaa ya Shinyanga James Msimba Ng'ombe akiwataka waandishi wa habari pia kujiendelea kielimu na kumtanguliza Mungu katika kazi zao.
Mkurugenzi wa Shirika la AGAPE mjini Shinyanga John Myola akipongeza waandishi wa habari kwa kushirikiana na Shirika hilo kikamilifu hasa kwenye kupigania haki za watoto na kupunguza matukio ya mimba na ndoa za utotoni.
Wafanya kazi wa Radio Faraja wakirusha matangazo moja kwa moja 'Mubashara' kwenye maadhimisho hayo ya uhuru wa vyombo vya habari mkoani Shinyanga.
Waandishi wa habari kutoka Radio Faraja Anastazia Paulo (kulia) akiwa na Flora Masalu wakiwa ukumbini
Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Zainab Telack (Katikati mwenye ushungi) akichukua mawili matatu ya kuyafanyia kazi siku hiyo ya uhuru wa vyombo vya habari.
Kamati ya ulinzi na usalama mkoa wa Shinyanga nayo ikisikiliza michango mbalimbali kwa makini siku hiyo ya maadhimisho ya uhuru wa vyombo vya habari mkoani Shinyanga ikiwemo tatizo la kukithiri kwa mauaji ya wanawake kwa kukatwa mapanga kutokana na imani za Kishirikina.
Mwandishi wa habari wa Gazeti la DailyNews Suleiman Shaghata akichangia mada kwenye maadhimisho hayo ya uhuru wa vyombo vya habari.
Mwenyekiti wa Chama cha ACT- Wazalendo mkoani Shinyanga Siri Yasini akiwataka waandishi wa habari kuutangaza mkoa hasa kwenye fursa ya viwanda.
Viongozi wa Klabu ya waandishi wa habari mkoani Shinyanga , wakiwa na kamati ya ulinzi na usalama Meza kuu, siku ya maadhimisho ya uhuru wa vyombo vya habari mkoani humo.
Maadhimisho yakiendelea .
Kamanda wa TAKUKURU mkoa wa Shinyanga Gasto Mkono akiwashauri waandishi wa habari mkoani humo kuanzisha miradi mbalimbali ya maendeleo ili kujikwamua kiuchumi, na kuacha kutumika ili kuandika habari za wanyonge.
Waandishi wa habari mkoa wa Shinyanga wakiwa kwenye maadhimisho hayo, wa kwanza mkono wa kulia ni Anikazi Kumbemba, mwandishi habari na mkurugenzi msaidizi wa kituo cha Radio Rafaja, Katikati ni Kareny Masasi mwandishi wa Gazeti la Habari Leo, akifuatiwa na Suzy Butondo Mwandishi wa Gazeti la Mwananchi.
Wadau wa habari wakiwa kwenye maadhimisho ya uhuru wa vyombo vya habari mkoani Shinyanga.
Wadau wa habari wakiwa kwenye maadhimisho ya uhuru wa vyombo vya habari mkoani Shinyanga.
Wadau wa habari wakiwa ukumbini.
Wadau wa habari wakiwa ukumbini
Wadau wa habari wakiwa ukumbini
Wadau wa habari wakiwa ukumbini.
Wadau wa habari wakiwa ukumbini


Wadau wakiwa ukumbini
Waandishi wa habari wakiwa kwenye maazimisho hayo ya habari mkoani Shinyanga.
Mwenyekiti wa Klabu ya waandishi wa habari mkoani Shinyanga Kadama Malunde, mkono wa kushoto akiwa na mkuu wa mkoa wa Shinyanga Zainabu Telack wakiteta jambo.
Mwenyekiti wa Klabu ya waandishi wa habari mkoani Shinyanga Kadama Malunde mkono wa kushoto akifurahia jambo wakati akizungumza na mkuu wa mkoa wa Shinyanga Zainabu Telack.
Kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa wa Shinyanga wakiwa kwenye picha ya Pomoja na wadau wa habari mkoani humo mara baada ya kumaliza kuazimisha siku hiyo ya uhuru wa vyombo vya habari mkoani hapa.
Waandishi wa habari mkoani Shinyanga wakipiga picha ya pamoja na kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa huo.
Wadau wa habari mkoani Shinyanga wakipiga picha ya pamoja na kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa huo.

Picha zote na Marco Maduhu - Shinyanga News Blog & Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527