RC KIGOMA AWAFUNDA WAANDISHI WA HABARI,ATAKA WAEPUKE HABARI ZA MATUKIO

Waandishi wa habari Mkoani Kigoma wametakiwa kufanya kazi kwa weledi na kuongeza ubunifu katika kazi zao ili kuchochea maendeleo ya mkoa wa Kigoma. 

Rai hiyo imetolewa  Mkoani Kigoma Katika kilele cha Maadhimisho ya uhuru wa Vyombo vya habari Duniani  'Mei 3' yaliyofanyika kimkoa katika Manispaa ya Kigoma Ujiji, ambapo mgeni Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Brigedia jenerali mstaafu Emanuel Maganga alisema uandishi wa habari za matukio umepitwa na wakati.

Alisema waandishi wenye taaaluma wanatakiwa kutumia kalamu zao kuandika habari zenye ubunifu na weledi mkubwa kwa kutafuta undani wa habari wanazoziandika.

Aidha Mkuu huyo aliwaasa Waandishi wa Habari kutumia taaluma yao kuwashawishi vijana wadogo kuipenda fani ya uandishi wa habari, kwa kuwatembelea wanafunzi shuleni na kutoa elimu juu ya fani hiyo ilikuepukana na fani hiyo kuonekana wanaoingia katika fani hiyo ni wale wanaoshindwa kutimiza ndoto zao kwa kuwa fani hiyo ni sawa na fani zingine.

"Tunaona fani ya uandishi wa habari imevamiwa na watu wengi sasa hivi tunaona kila mtu ana uwezo wa kuripoti matukio kwa kutumia mitandao ya kijamii kutokana na utandawazi uliopo kwa sasa, kama wana habari lazima tuwe wabunifu sana katika kuripoti habari na matukio kwa kuwashawishi wasomaji na watazamaji kuona kweli fani hii ina utofauti na matukio mengine", alisema Maganga.


Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa habari Mkoani wa Kigoma (KGPC) Adela Madyane alisema chama cha Waandishi wa habari kina mpango wa kuwaunganisha Waandishi wa habari wote Mkoani Kigoma ili kuhakikisha Waandishi wanakuwa na maadili na kuzingatia misingi ya uandishi wa habari.

Alisema Klabu inaendelea kusimamia misingi na taratibu za kitaaluma zilizowekwa kisheria ili kuondoa migogoro baina ya Wanahabari na wadau wa maendeleo, na wanachama wenye vigezo ili kuepuka waandishi wasio na taaluma.


Nae Katibu wa KGPC Fadhili Abdallah alisema Waandishi wa habari watahakikisha wanashirikiana na wananchi na viongozi katika kuhakikisha wanaripoti habari zenye tija na maendeleo kwaajili ya kuuinua mkoa wa Kigoma.

Alisema Changamoto wanazokutana nazo ni pamoja na baadhi ya viongozi na wadau kuzuia baadhi ya taarifa na kuwanyima ushirikiano Waandishi wa habari pindi wanapohitaji taarifa na kuomba viongozi wote kutoa ushirikiano kwakuwa Waandishi wa habari wana mchango mkubwa wa kuinua maendeleo hasa katika mikoa ambayo bado iko nyuma.
Na Rhoda Ezekiel - Malunde1 blog
Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Brigedia jenerali mstaafu Emanuel Maganga akizungumza wakati wa maadhimisho ya siku ya uhuru wa vyombo vya habari mkoani Kigoma - Picha na Rhoda Ezekiel - Malunde1 blog




Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527