MUUZA PEMBA ABAKA MTOTO KWA AHADI YA MAANDAZI SHINYANGA


Jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga linamshikilia Amos Meshack (36) mfanyabiashara wa udongo wa Pemba kwa tuhuma ya kumbaka mtoto mwenye umri wa miaka 9 mwanafunzi wa darasa la pili katika shule ya msingi Ndala A katika manispaa ya Shinyanga. 

Tukio hilo limetokea Aprili 30,2018 majira ya saa saba mchana nyumbani kwa mtuhumiwa huyo katika kata ya Ndala manispaa ya Shinyanga. 

Akisimulia kuhusu tukio hilo mama mzazi wa mtoto huyo alisema aligundua mwanae huyo amebakwa mara baada ya kuona nguo zake za ndani zikiwa zimefichwa nyuma ya kitanda, huku chupi ikiwa na damu pamoja na mbegu za kiume na yeye kuonekana kuwa mnyonge. 

Alisema baada ya kumbana mtoto huyo alisema kuwa amebakwa na Baba Amani ambaye ndiye Amos Meshack, na kuwa huo ndio mchezo wake wa kila siku ambapo wakati akianza uchafu huo alikuwa akimpatia pipi, na safari hii alimnunulia maandazi na kisha kumvutia ofisini kwake na kumbaka tena. 

“Baada ya mwanangu kumtaja mwanaume huyo nilitoa taarifa Polisi pamoja na kwa Mwenyekiti wa mtaa kisha tukaenda eneo la tukio kumkamata mtuhumiwa ambapo alimbakia kwenye ofisi yake ya kutengenezea Pemba”, alielezea mama huyo. 

“Pia nilimpeleka kwenye hospitali ya rufaa ya mkoa wa Shinyanga kwenda kupimwa, na majibu ya daktari yalivyotoka ilibainika kweli mwanangu amebakwa na mchezo huo amekuwa akifanyiwa kila mara na siyo mara moja, na hali yake anaendelea vizuri,”aliongeza. 


Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga,ACP Simon Haule alisema chanzo cha tukio hilo ni tamaa za kimwili ambapo mbinu iliyotumika ni mtuhumiwa kumwita mtoto huyo kwa ahadi ya kumpatia shilingi mia mbili kwa ajili ya kununulia maandazi. 

“Kutokana na ahadi hiyo,mtoto aliingia katika nyumba/kibanda ambacho mtuhumiwa hukitumia kufanyia biashara ndogo ndogo za kufinyanga na kutengeneza udongo aina ya Pemba ndipo alimkamata na kumbaka akimsisitiza asieleze chochote kwa mtu yeyote”,alieleza Kamanda Haule. 

“Hata hivyo mama mzazi wa mtoto huyo aligundua tukio la kubakwa kwa mwanae baada ya kumuona akiwa hana furaha na kuamua kumdadisi”,aliongeza. 

Kamanda Haule alisema wanamshikilia mtuhumiwa na baada ya uchunguzi wa awali kukamilishwa atafikishwa mahakamani. 

Na Kadama Malunde - Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527