ABDUL NONDO AMKATAA HAKIMU

Mshtakiwa katika kesi ya kujiteka na kusambaza taarifa za uongo katika mitandao ya kijamii, Abdul Nondo ameandika barua ya kumkataa Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mkoa wa Iringa, John Mpitanjia, anayesikiliza kesi hiyo kwa madai ya kuwa karibu na Mkuu wa Upelelezi wa Polisi Mkoa wa Iringa.


Wakili anayemtetea Nondo, Jebra Kambole ametoa sababu tano za mteja wake kuandika barua hiyo tangu Mei 11, mwaka huu za kumkataa hakimu huyo ikiwamo hakimu huyo kuonekana akiingia katika gari la Mkuu wa Upelelezi na kwenda sehemu isiyojulikana, ambapo kutokana na hali hiyo, mteja wake ameona haki haitatendeka.


Amedai sababu nyingine ni hakimu huyo kukutwa amekaa na Paul Kisapo ambae ni shahidi wa tatu katika kesi hiyo.


Kwa upande wake Wakili Upande wa Jamhuri, Abel Mwandalama amedai pamoja na kupokea barua ya mshtakiwa kumkataa hakimu lakini ameona hayana msingi katika kesi hiyo.


“Tunasema hayo kwa kuwa Aprili 19, shahidi wa tatu katika shauri hilo alitoa ushahidi wake na mshitakiwa hakuandika barua yoyote na hata kesi hiyo ilipokuja tena Mei 10, mwaka huu hakuna barua iliyoandikwa iweje barua hiyo kuandikwa Mei 11, baada ya mahakama hiyo kukubali vielelezo vilivyotolewa na upande wa jamhuri kutumika kama ushahidi,” amedai Wakili Mwandalama.


Baada ya kusikiliza hoja za pande zote mbili, Hakimu Mpitanjia alisema uamuzi wa kujitoa ama kuendelea na kesi hiyo utatolewa Mei 16, mwaka huu.


Nondo anakabiliwa na mashtaka mawili ambayo ni kusambaza taarifa za uongo akiwa Ubungo jijini Dar es Salaam, na kutoa taarifa za uongo akiwa mjini Mafinga kwa askari Polisi kituo cha Mafinga Wilayani Mufindi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527