ALIKIBA AIBUKIA WASAFI KWA DIAMOND PLATNUMZ



Kama ulikuwa unadhani nyimbo za Alikiba hazitachezwa katika televisheni ya Wasafi inayomilikiwa na Kampuni ya WCB utakuwa umekosea sana.

Leo Jumatano Aprili 4, 2018 televisheni hiyo ambayo ofisa mtendaji wake mkuu ni Nassib Abdul maarufu Diamond Platnumz imecheza nyimbo za Alikiba.

Televisheni hiyo inayoonekana katika king’amuzi cha Azam ilianza majaribio ya kurusha matangazo yake Aprili 2, 2018.

Kuchezwa kwa nyimbo za Alikiba ni wazi kutakuwa kumewapa jibu wapenzi wa muziki wa Bongo Fleva nchini kutokana na kwamba wawili hao mara kwa mara kuelezwa kuwa na ushindani.

Mambo ni tofauti. Nyimbo mbalimbali za Alikiba kwa siku nzima ya leo zimekuwa zikipigwa katika televisheni hiyo.

Mwandishi nguli wa habari za michezo wa Kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL) inayochapisha magazeti ya Mwananchi, MwanaSpoti na The Citizen, Edo Kumwembe kupitia ukurasa wake wa Instagram jana aliweka ujumbe uliozua mjadala.

Ujumbe huo ulioambana na picha ya logo ya Wasafi TV unasomeka, “Naam Watazamani wetu wa Wasafi TV katika countdown yetu leo wimbo ulioshika namba moja ni Seduce Me kutoka kwa Ali Kiba.”

Baadhi ya wachangiaji waliungana na Edo na wengine walimpinga lakini leo Edo tena kupitia ukurasa wake huo, ameweka ujumbe ukiambatana na picha aliyoipiga ikionyesha wimbo wa Ali Kiba ukipigwa kwenye Wasafi TV.

Edo amesema, “Jana watu walitoka povu humu…anyway Diamond Platinum ni Professional musician na mfanyabiashara anayejua anachokifanya.”

Na Ibrahim Yamola, Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527