YANGA YACHEZESHWA MAKHIRIKHIRI..YAKUBALI KIPIGO CHA 2 - 1 MCHEZO NA TOWNSHIP ROLLERS


Klabu ya soka ya Yanga imekubali kipigo cha mabao 2-1 kutoka kwa timu ya Township Rollers ya Botswana kwenye mchezo wa ligi ya Mabingwa Afrika uliomalizika uwanja wa taifa jijini Dar es salaam leo jioni Machi 6,2018.

Township Rollers ndiyo walikuwa wa kwanza kuandika bao la kuongoza dakika ya 11 kipindi cha kwanza lililofungwa na Lemponye Tshireletso kabla ya Yanga kusawazisha dakika ya 30 kupitia kwa Obrey Chirwa hivyo hadi mapumziko timu zilitoshana nguvu.

Kipindi cha pili Yanga ilianza kushambulia kwa kasi huku Township wakionekana kujilinda kabla ya kutumia shambulizi la kushitukiza na kuandika bao la pili dakika ya 83 kupitia kwa Motsholetsi Sikele na kupunguza matumaini ya Yanga kuwania kitita cha bilioni 1.1 ambacho hutolewa na CAF kwa timu inayotinga hatua ya makundi.

Baada ya mchezo wa leo timu hizo zitarudiana tena Machi 17,2018 ambapo Yanga itasafiri hadi jijini Gaborone Botswana kwa ajili ya mchezo huo huku ikiwa na deni la kushinda mabao 2-0 au zaidi ili kujihakikishia inatinga hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527