HALMASHAURI YA WILAYA YA KILWA YAGAWA BURE MICHE YA KOROSHO KWA WAKULIMA


Katika kuongeza uzalishaji wa korosho kwa wakulima wa wilaya ya Kilwa, mkoa wa Lindi, halmashauri ya wilaya hiyo imewagawia miche ya korosho bila malipo.

Akisoma taarifa kwa mgeni rasmi wakati wa hafla ya ugawaji miche hiyo iliyofanyika leo katika kituo cha wanyama kazi cha Mkwanyule kilichopo katika mamlaka ya mji mdogo wa Kilwa Masoko, ofisa kilimo wa halmashauri hiyo, John Mkinga alisema jumla ya miche 772,000 iligawiwa bure kwa wakulima.

Mkinga ambaye alisoma taarifa hiyo kwa niaba ya mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, Zabron Bugingo, alisema wilaya hiyo inahekata hekata 509,040 zinazofaa kulimwa zao hilo.

 Hata hivyo ni hekta 9,420 pekee zilizolimwa zao hilo, zikiwa na mikorosho 650,000 yenye uwezo wa kuzalisha 3,944,821 hadi 5,677,000 kwa mwaka. Huku akibainisha kwamba ugawaji huo ni kwa ajili ya kuongeza uzalishaji.

Alisema katika msimu wa 2016 /2017 lengo la halmashauri hiyo lilikuwa ni kuzalisha miche 50,000,ilivuka lengo na kuzalisha miche 55,000 ambapo katika msimu huu wa 2017 /2018 lengo lilikuwa ni kuzalisha miche 1,122,000 hata hivyo imezalisha miche 772,000 iliyobebeshwa.

 "Kutofikiwa lengo kumetokana na uhaba wa mbegu, miche tuliyozalisha kulingana na mbegu tulizokuwa nazo ni hii 772000 ambayo leo tunagawa kwa wakulima, "alisema Mkinga.

Mkuu huyo wa idara ya kilimo alisema matarajio ya halmashauri hiyo ni kuwa na mikorosho 1,477,000 ndani ya kipindi cha miaka minne, ambayo itazalisha tani 9,812 kila mwaka.

Mkinga alizitaja baadhi ya changamoto zinazokwamisha kufikia malengo wanayojiwekea kuwa ni bodi ya korosho kushindwa kulipa 30% ya gharama za uzalishaji ambayo inasababisha kazi ya kuzalisha miche kutokamilika kwa wakati, bodi ya korosho kutoshiriki usambazaji wa miche vijijini. 

Hali inayosababisha wakulima wanaoishi mbali na vituo kushindwa kupata miche kwa wakati. 

Aliitaja changamoto nyingine kuwa ni bodi ya korosho kutopeleka kiasi cha mbegu kinacholingana na mahitaji. Hali inayosababisha Kutofikiwa lengo la uzalishaji. 

Kwa upande wake, mgeni rasmi kwenye hafla hiyo, mkuu wa wilaya ya Kilwa,Christopher Ngubiagai alitoa wito kwa wakulima kuchangamkia miche hiyo ili waongeze vipato vyao na taifa huku akiwaasa kutunza mashamba yao kwa kufanyia palizi kila mwaka ili miche hiyo isiungue moto kwani gharama iliyotumika kuzalisha ni kubwa na serikali inania njema kwao.



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527