DC LINDI AAGIZA VIONGOZI WA CHAMA CHA USHIRIKA WAKAMATWE KWA KUCHANGANYA MCHANGA NA KOROSHO


Mkuu wa wilaya ya Lindi, Shaibu Ndemanga ameliagiza jeshi la polisi wilayani humo liwakamate na kuwafikisha mahakamani viongozi na watendaji wa chama cha msingi cha ushirika cha ushirika Pangatena kwa tuhuma za kuchanganya mchanga na korosho (kuchakachua). 

Akieleza tukio hilo leo kutoka Lindi, alisema viongozi na watendaji wa chama hicho wanatuhumiwa kuchanganya mchanga na korosho baada ya kupokea kutoka kwa wakulima kwa lengo la kulinganisha uzito baada ya kupunguza na kuuza korosho walizopunguza.

 "Tuna kikosi kazi tumeunda kwa ajili ya kusimamia usafirishaji baada ya kununuliwa. Tulibaini kwamba kwenye ghala la Bucco kulikuwa na korosho zenye walakini. Tukafuatilia nakubaini zilikuwa korosho zilizotoka katika AMCOS ya Pangatena, takribni tani hamsini ambazo zilikuwa tayari kusafirishwa nje ya nchi, "alisema Ndemanga.

Alibainisha kuwa wanaofanya mchezo huo ni viongozi na watendaji wa vyama vya msingi vya ushirika baada ya kupokea korosho kutoka kwa wakulima. Ndipo wanapunguza na kujaza mchanga ili kufidia walizochota na kuuza kwa majina yao au ndugu na rafiki zao. 

"Licha ya kusababisha mgogoro baina ya wakulima na serikali lakini iwapo korosho zile zingekwenda nje ya nchi wangekuwa wameharibu soko la zao hilo na tungefedheheka, "alisema kwa masikitiko Ndemanga. 

Mkuu huyo wa wilaya aliongeza kusema licha ya kusitukia mchezo huo na kunusuru nchi kuingia kwenye fedheha lakini pia wamesababisha mgogoro wa malipo ya wakulima. 

Kwa madai kwamba ni vigumu wafanyabiashara walionunua korosho hizo kulipia na uzito wa mchanga waliongeza watendaji na viongozi wa chama hicho. 

Hata hivyo wakulima watataka walipwe kwa mujibu wa uzito halali unaonekana kwenye stakabadhi zao za mauzo.

"Niwatu hatari sana wale, niliagiza wakamatwe na wafikishwe mahakamani. Tayari watendaji na wajumbe wa bodi wa chama hicho wapo mahabusu," alisema Ndemanga. 

Wilaya ya Lindi imekuwa na rekodi mbaya ya uaminifu kupitia vyama vya ushirika vya msingi. ambapo miaka mitatu iliyopita ziliporwa fedha takribani shilingi milioni 400 za malipo ya wakulima wa korosho waliokuwa wamepeleka kwenye chama cha msingi cha ushirika cha NANYUM. 

Hata hivyo mazingira ya uporwaji wake yaliibua maswali mengi yaliyokosa majibu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527