AUAWA KWA KUNYONGWA NA MPENZI WAKE KWA WIVU WA KIMAPENZI


WATU watatu wamefariki dunia katika siku ya mkesha wa Krismasi wilayani Tarime mkoani Mara, wakiwemo mwanamke Robhi Magaigwa (36) aliyeuawa kwa kunyongwa kwa sababu za wivu wa kimapenzi.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi, Kanda Maalumu ya Tarime Rorya, Henry Mwaibambe alitaja matukio mengine mawili ya vifo kuwa ni pamoja na Nyamboge Kegokora (93) aliyekufa baada ya kukanyagwa na lori la mchanga na dereva wa bodaboda Nankongo Makanda (32) aliyepata ajali ya pikipiki na kufa papo hapo.

Alisema katika tukio la kwanza mkazi wa Ronsoti, Magaigwa aliuawa kwa kunyongwa shingo na mtu anayedaiwa kuwa mpenzi wake Chacha Mangiti ama kwa jina lingine Peter Irondo.

Alieleza kuwa katika taarifa za awali, sababu za kifo hicho zinadaiwa kuwa ni wivu wa mapenzi na tayari mtuhumiwa amekamatwa, kuhojiwa na anasubiriwa kupandishwa kizimbani.

Akizungumzia kifo cha Kegokora, Kamanda Mwaibambe alisema Desemba 25, gari aina ya Fuso lenye namba za usajili T 766 DJN lililokuwa likiendeshwa na mmliki wa gari hilo, Chacha Borega lilimkanyaga mzee huyo aliyekuwa amekaa kando ya barabara.

Alisema pamoja na tukio hilo pia siku hiyo ya Desemba 25, mwendesha bodaboda mkazi wa Kijiji cha Pemba tarafa ya Inchugu, Makanga alipata ajali wakati akiendesha pikipiki yake kwa mwendokasi na kupatwa na mauti.

Alisema chanzo cha ajali hiyo ni kikoi alichokuwa amevaa kunasa kwenye rimu ya tairi ya pikipiki yake na kusababisha pikipiki hiyo ipinduke ambapo mwendesha bodaboda huyo, alikufa kutokana na majeraha makubwa aliyopata kichwani.

IMEANDIKWA NA SAMSON CHACHA - Habarileo TARIME

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527