BABA MTAKATIFU FRANCISCO AMTEUA ASKOFU ISAAC MASSAWE KUWA ASKOFU MKUU JIMBO KUU LA ARUSHA


Askofu Isaac Amani Massawe
***

Baba Mtakatifu Francisko amekubali ombi lililowasilishwa kwake na Askofu mkuu Josephat Louis Lebulu wa Jimbo kuu la Arusha, Tanzania la kustaafu kutoka madarakani. 

Wakati huo huo, Baba Mtakatifu amemteua Askofu Isaac Amani Massawe wa Jimbo Katoliki Moshi, kuwa Askofu mkuu mpya wa Jimbo Kuu la Arusha, Tanzania. 

Askofu mkuu mteule Isaac Amani Massawe, alizaliwa tarehe 10 Juni 1951 huko Mango, Jimbo Katoliki la Moshi. 

Baada ya masomo na majiundo yake ya kikasisi, akapadrishwa kunako tarehe 29 Juni 1975.

Tarehe 21 Novemba 2007 akateuliwa na Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto XVI kuwa Askofu wa Jimbo Katoliki Moshi na kuwekwa wakfu tarehe 22 Februari 2008 na Kardinali Polycarp Pengo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam akisaidiana na Askofu mkuu Josephat Louis Lebulu wa Jimbo kuu la Arusha pamoja na Hayati Askofu Amedeus Msarikie wa Jimbo Katoliki la Moshi. 

Hivi karibuni, aliteuliwa pia kuwa ni Msimamizi wa Kitume Jimbo Katoliki la Mbulu.

Kwa ufupi, Askofu mkuu mteule Isaac Amani Massawe alisoma shule ya msingi Mango, Kibosho; Seminari ndogo ya St. James, Moshi; Falsafa kati ya mwaka 1970 – 1972, Seminari kuu ya Ntungamo, Jimbo Katoliki Bukoba. 

Alijipatia masomo ya Taalimungu Seminari kuu ya Kipalapala, Jimbo kuu la Tabora kati ya mwaka 1972 – 1975 na hatimaye, kupadrishwa mwezi Juni 1975. Kama Padre aliwahi kuwa Paroko usu, mwalimu na mlezi wa Seminari ndogo ya St. James, Moshi.

Kati ya Mwaka 1986 hadi mwaka 1989 alikuwa masomoni, Chuo kikuu cha Walsh, nchini Marekani; kati ya mwaka 1990 hadi mwaka 2003, mlezi wa watawa na baadaye akateuliwa kuwa ni Paroko wa Kanisa kuu la Kristo Mfalme, Jimbo Katoliki la Moshi.


Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Chanzo : Radiovaticana

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527