DIALLO AKERWA GARI LAKE KUPEKULIWA NA TAKUKURU AKIOMBA KURA UCHAGUZI WA CCM





Mwenyekiti wa CCM mkoani Mwanza, Anthony Diallo amedai kukerwa na kitendo cha maofisa wa Takukuru kusimamisha gari lake na kulipekua, wakati alipokuwa kwenye harakati za kampeni wilayani Ukerewe.

Mfanyabiashara huyo maarufu Kanda ya Ziwa anatetea nafasi yake katika uchaguzi uliofanyika jana.


Hali hiyo, imekuja wakati uchaguzi wa viongozi wa CCM ukiwa umefikia ngazi ya mkoa huku katika baadhi ya mikoa kukiwa na malalamiko mengi ya rushwa.

Akizungumza wakati akiomba kura jana, Diallo alisema amesikitishwa na kutofurahishwa na kitendo cha maofisa hao.

“Kitendo hiki (cha gari kupekuliwa), hakikuwa cha kiungwana,” alisema Diallo ambaye anamiliki kampuni ya Sahara Media inayomiliki kituo cha televisheni na redio.

“Hata mimi najua rushwa ni adui wa haki na nimeahidi kupambana na rushwa kwa ahadi na imani ya mwana CCM.”

Mbali na kupekua gari la waziri huyo wa zamani, Takukuru iliwahoji baadhi ya wagombea na wanachama mkoani Simiyu kwa tuhuma za rushwa.

Wakati mkuu wa Takukuru mkoani Mwanza, Ernest Makale akithibitisha kupekuliwa kwa gari la Diallo, mwenzake wa Simiyu, Adili Elinipenda amesema taasisi yake inawashikilia viongozi na wanachama kadhaa kwa mahojiano.

Wakuu hao wawili wamethibitisha matukio hayo walipozungumza na Mwananchi kwa njia ya simu jana.

Kuhusu gari la Diallo kupekuliwa, Makale alisema tukio hilo lilitokea wilayani Ukerewe baada ya maofisa wa Takukuru kupata taarifa kuwa kiongozi huyo aliyekuwa wilayani humo kufanya kampeni alikuwa akijihusisha na vitendo vya rushwa.

“Hata hivyo, baada ya kulisimamisha gari yake na kufanya upekuzi, hatukukuta ushahidi wowote na kumuachia kuendelea na kampeni zake,” alisema Makale.

Diallo aliyewahi kuwa Waziri wa Maliasili na Utalii katika Serikali ya Awamu ya Nne, ni miongoni mwa wagombea waliopitishwa na Halmashauri Kuu kutetea nafasi yake.

Katika tukio la Simiyu, Elinipenda alisema Takukuru inaendelea kuwahoji baadhi ya viongozi na wanachama wa CCM lakini hakuwa tayari kuwataja.

“Nitatoa taarifa na kutaja majina ya tunaowahoji baada ya zoezi la kuwahoji kukamilika,” alisema Elinipenda.

Na Johari Shani na Faustine Fabian mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527