ASKARI POLISI AMUUA ASKARI WA JWTZ KWA KUMPIGA RISASI


Askari wa kike wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) Kikosi cha 514 KJ Makambako mkoani Njombe, ameuawa kwa kupigwa risasi na mchumba wake ambaye ni askari wa Jeshi la Polisi, Inadaiwa kuwa tukio hilo, lilitokana na kuibuka ugomvi kati yao.


Inadaiwa askari huyo namba H 2299 Zakaria Dotto, alimpiga risasi mbili mchumba wake, Neema Masanja (25) mkazi wa Mtaa wa Jeshini Kata ya Maguvani Halmashauri ya Mji wa Makambako mkoani Njombe, baada ya kuibuka ugomvi kati yao saa 12 jana Desemba 27,2017 alfajiri.


Wakizungumza katika eneo la tukio, majirani wa marehemu walisema majira ya alfajiri walisikia risasi zikirindima katika chumba cha marehemu na walipoangalia nje ya nyumba hiyo walimuona mdogo wake akimkimbiza mtu ambaye hawakumuona sura.


Mmiliki wa nyumba hiyo ambayo marehemu alikuwa amepanga, Asty Lusambo, alisema alisikia kishindo cha risasi na alipofungua dirisha akiwa na mkewe, walimuona mdogo wa marehemu akimkimbiza mtu.


Mke wa Lusambo, Sophia Manyika, alisema alimfuata mdogo wa marehemu na baadaye alimkuta katika msitu wa Jeshi akiwa amechoka na chini yake kukiwa na bunduki aina ya SMG ambayo ilitupwa na mtuhumiwa wa mauaji hayo na kupotelea msituni.


Ofisa Mtendaji wa Mtaa wa Jeshini, Afrah Mbunju, alisema tukio hilo lilitokea mtaani kwake na alipofika eneo la tukio alisimuliwa na mashuhuda kuhusiana na kilichotokea.


Mtendaji huyo alieleza kuwa wawili hao walikuwa wachumba ambao ni wakazi wa mtaa wake.


“Mwanaume ambaye ni askari wa Jeshi la Polisi alikuwa anatakiwa kwenda lindo latika moja ya taasisi za kifedha ambapo alimkuta huyo binti nyumbani kwake akijiandaa kwenda kazini, ndipo ukaibuka ugomvi na marehemu amekutwa akiwa na mikwaruzo shingoni akiwa ameuawa,” alisema Mbunju.


Alisema askari hao ni wakazi wa kijiji kimoja mkoani Mwanza na walikuwa wanatarajia kuoana kwa kuwa mwanaume alikuwa ameshapeleka mahari.


Aliongeza: “Walikuwa ni wachumba tayari miezi michache iliyopita wametoleana mahari na walikuwa wanatarajia kuoana Februari mwakani.”


Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Makambako, Dk. Kesha Mgunda, alithibitisha kuupokea mwili wa marehemu kwa ajili ya uchunguzi na baada ya uchunguzi waliukabidhi kwa ndugu wa marehemu ambao wameuhifadhi katika hospitali ya Ilembula kwa ajili ya taratibu za maziko.


Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Njombe, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Pudensiana Protas, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kuwa mtuhumiwa alikuwa kazini, lakini alitoroka lindo kabla ya tukio hilo.


Alisema Jeshi hilo linaendelea na msako wa askari huyo na kuwataka wananchi kutoa taarifa popote watakapomuona.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527