WATU 40 WAUGUA KWA KULA KIPORO CHA UGALI MSIBANI KAHAMA


WATU 40 wa Kitongoji cha Isumbi katika Kijiji cha Igung’hwa Kata ya Kinaga katika Halmashauri ya Mji wa Kahama mkoani Shinyanga, wamelazwa katika Hospitali ya Wilaya hiyo baada ya kinachodaiwa kuwa ni kula kiporo na mboga za majani aina ya mgagani.

Ofisa Mtendaji wa Kata ya Kinaga, Paul Damasi alisema wananchi waliolazwa katika Hospitali ya Mji wa Kahama ni wale waliokula kiporo cha ugali na mboga za majani aina ya mgagani waliouita “mchicha.”

Aliyasema hayo juzi wakati akizungumza na wananchi katika msiba uliotokea nyumbani kwa Salum Manyanda na kuongeza kuwa asilimia kubwa ya watu waliougua ghafla baada ya kula chakula hicho ni wanawake.

Ofisa Mtendaji wa Kata huyo alisema tukio hilo lilitokea juzi saa tano asubuhi baada ya waombolezaji kula chakula kilichobakia jana ya siku hiyo huku akieleza kuwa wote waliougua ghafla walikimbizwa katika hospitali ya Wilaya ya Kahama kupatiwa matibabu.

“Idadi ya watu haijafahamika ila nimepewa taarifa kuwa ni zaidi ya wakinamama arobaini ndiyo waliokimbizwa katika Hospitali ya Mji wa Kahama, msiba ulitokea Novemba 14, kama unavyojua vijijini bado kuna ile tabia ya msiba unapotokea akinamama wanapika chakula nyumbani kisha wanapeleka msibani.

“Ule ugali uliobaki siku ya kwanza ya msiba ulikosa mboga ikabidi wakina mama waingie katika mashamba kuchuma mboga ambapo walipika mboga aina mbili mrenda na mgagani uliodaiwa kuwa ni mchicha, sisi wanaume tulikula ugali na mrenda akina mama wakala ugali na hiyo mboga ya mgagani ndiyo chanzo cha tukio,” alisema.

Naye Joyce Samweli alilieleza kuwa wakati wakipeleka chakula kingine katika msiba huo uliodumu siku mbili, alikutana na akinamama wenzake waliougua ghafla ugonjwa huo wakionekana kukosa nguvu, kuangua vicheko na kukimbia ovyo jambo lililoushangaza umati msibani.

IMEANDIKWA NA RAYMOND MIHAYO, KAHAMA

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527