WANAFUNZI WA ELIMU YA JUU WALIOKOSA MIKOPO WAANDAMANA HADI BODI YA MIKOPO DAR


Baadhi ya wanafunzi waliochaguliwa kujiunga na vyuo vya elimu ya juu wamekwenda ofisi za Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) kushinikiza wapewe mikopo ili wafanye usajili kwa mwaka wa masomo 2017/18.

Wanafunzi hao wamekusanyika leo Jumatatu Novemba 6,2017 katika ofisi za HESLB zilizoko Mwenge jijini Dar es Salaam, hivyo kusababisha askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) kufika eneo hilo.

Baadhi ya wanafunzi waliangua vilio walipozungumzia tabu wanazopata kutokana na majina yao kutoonekana katika orodha ya wanaopata mikopo.

Soma: HESLB yatoa orodha ya wanafunzi waliopangiwa mikopo

Mwanafunzi, Nillan Liunga amesema hajui hatima yake kwa kuwa fedha alizonazo zinakaribia kwisha na hana ndugu jijini Dar es Salaam.

"Maisha yenyewe naishi ya kuungaunga nimetoka Mbeya nimefikia gesti. Sina wazazi, nimesoma kwa shida licha ya kuwa na vigezo vyote vya kupewa mkopo mpaka sasa sijui nini hatima yangu," amesema Liunga.

Wanafunzi hao wametakiwa na maofisa wa HESLB kuorodhesha majina yao jambo ambalo wamesema halijawaridhisha.

"Kama tulituma maombi mtandaoni hawajatupa mkopo, hayo majina ya kwenye karatasi watayatumia kweli? au ndiyo wanatudanganya," amehoji mwanafunzi Christopher Mwita.

Mwita amesema kwa chuo alichochaguliwa anatakiwa kulipa asilimia 50 ya ada ili asajiliwe na muda wa usajili unakwisha ndiyo maana amefika ofisi za HESLB kujua hatima yake.

"Ijumaa ndiyo usajili unafungwa lakini sisi tumeambiwa tusubiri Jumatatu ndipo watatangaza utaratibu wa kukata rufaa," amesema Mwita.

Mkurugenzi wa Mawasiliano wa HESLB, Omega Ngole amesema jukumu lao ni kuwapokea na kusikiliza hoja za wanafunzi hao kabla ya kuzifanyia kazi.

Soma: Wanafunzi wote wenye sifa kupewa mikopo chuo kikuu

Amesema wamewataka wanafunzi hao kuorodhesha majina ili waangalie ni wapi walikosea na kuwapa majibu au kufanyia kazi changamoto zao.

“Tunaendelea kuifanyia kazi orodha ya majina tuliyopokea kutoka Tume ya Vyuo Vikuu (TCU). Majina wanayoandika leo pia tutayafanyia kazi, hadi Ijumaa tutatoa orodha ya nne ya wanufaika wa mikopo wenye sifa,” amesema Ngole.

Amesema wanafunzi wanaolalamika ikibainika kuna wenye sifa za kupata mkopo kutokana na vigezo vilivyotajwa, wameomba kwa usahihi na wameambatanisha kila kinachohitajika, watasaidiwa kwa kila hali.

“Wiki ijayo tutafungua rasmi dirisha la kukata rufaa, hivyo wanafunzi wenye malalamiko yakiwemo ya kupata mikopo midogo na kunyimwa ilihali wanastahili watapata fursa ya kusikilizwa,” amesema Ngole.

Source: Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527