TAHADHARI KUHUSU UJIO WA MVUA KUBWA MAENEO MBALIMBALI NCHINI

Mamlaka ya Hali ya Hewa (TMA), imewatahadharisha wadau, wanajamii na sekta zinazojishughulisha na mazingira juu ya mafuriko yanayoweza kutokea katika kipindi cha mvua za msimu zinazotarajiwa kuanza kunyesha kati ya mwezi Novemba na Aprili 2018.

Mkurugenzi wa Mamlaka ya Hali ya Hewa, Dkt. Agnes Kijazi ameeleza hayo leo Jumanne, Oktoba 17, na kusema kuwa katika kiipindi hicho kunatarajiwa kuwa na vipindi vifupi vya mvua kubwa katika maeneo mbalimbali nchini ambavyo vinaweza kusababisha mafuriko katika baadhi ya maeneo.

Dkt. Kijazi amewataka wadau wa sekta mbalimbali zinazohusiana na mazingira kufuatilia kwa ukaribu taarifa za hali ya hewa zinazotolewa ili kuondokana na madhara yanayoweza kuepukika.

“Wadau wa sekta ya uvuvi, kilimo, mifugo, chakula na wanyamapori wanatakiwa kufuatilia kwa ukaribu taarifa za hali ya hewa. Kufahamu mapema kutasaidia kujipanga,” alisema Dkt. Kijazi.

Aliongeza kuwa kufuatia mvua hizo zinazotarajiwa, kiwango cha unyevu katika udongo kitaongezeka na hivyo kuwataka wachimbaji wa wadogo wa madini kuchukua tahadhari kwani unyevu huo unaweza kupelekea mmomonyoko wa ardhi na kuleta maafa.

Aidha, amezitaka mamlaka za miji na sekta mbalimbali kuhakikisha wanafanya ukaguzi wa mitaro na mifereji ya kupitisha maji iwe inafanya kazi muda wote ili kuepusha kutuama kwa maji na kusababisha mafuriko pamoja na maonjwa ya milipuko.

“Sekta ya afya ichukue hatua stahiki ili kupunguza athari zinazoweza kujitokeza kutokana na vipindi vifupi vya mvua kubwa vinavyoweza kusababisha milipuko ya magonjwa,” amesema Dk Kijazi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post