KIGWANGALA AFUTA VIBALI VYOTE VYA UWINDAJI

Waziri wa Maliasili na Utalii, Hamisi Kigwangalla amefuta vibali vyote vya uwindaji kwa kampuni kuanzia Oktoba 22,2017 na kutoa siku 60 kwa watendaji ili waratibu mchakato upya utakaowezesha vitalu kugawiwa kwa mnada.


Dk Kigwangalla pia amemwagiza katibu mkuu wa wizara hiyo, ndani ya muda mfupi kuwaandikia Hazina ili kuzichukua hoteli 10 kati ya 17 zilizobinafsishwa ambazo zimeshindwa kutimiza masharti.


Ametoa maagizo hayo jana alipohitimisha mazungumzo na wadau wa sekta ya utalii na maliasili aliokutana nao mjini Dodoma.


“Kwa mamlaka niliyonayo katika sheria, natamka kwamba, nafuta rasmi vibali vyote vya uwindaji kwa kampuni vilivyotolewa na wizara yangu kwa mwaka huu. Pia, naagiza watendaji wote wanaosimamia hili wahakikishe wanaandaa mchakato ndani ya siku 60 ili mnada ufanyike na uwe wa uwazi,” aliagiza Dk Kigwangalla.


Kuhusu vitalu vyenye migogoro vikiwemo vya Loliondo na Natroni, ameagiza visigawiwe hadi migogoro itakapokwisha.


"Kwenye hili la hoteli, nataka katibu uwasiliane na mamlaka husika, ikiwemo Msajili wa Hazina ili ndani ya siku 60 uje na majibu tutangaze kwa wawekezaji watakaokwenda na masharti," amesema.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527