RUNGWE AMTEMBELEA GODBLESS MAHABUSU

Mwenyekiti  wa Chama cha Ukombozi wa Umma (Chauma), Hashim Rungwe, amemtembelea Mbunge wa Arusha Mjini, Godbles Lema (Chadema), ambaye   bado yuko mahabusu katika Gereza la Kisongo mkoani Arusha.

Akizungumza na waandishi wa habari  mjini Arusha jana baada ya kuonana na mbunge huyo, Rungwe alisema baadhi ya matatizo yanayotokea kwenye jamii yanasababishwa na baadhi ya watawala.

Alisema hali hiyo imekuwa ikiibua chuki miongoni mwa wananchi   jambo ambalo si zuri na linahitaji kukemewa.

Kiongozi huyo alimtembelea Lema    akiwa  amefuatana  na viongozi mbalimbali akiwamo Makamu Mwenyekiti wa Chauma, Kayumbo Kabutali  na wabunge wa Bukoba Mjini, Wilfred Lwakatare na Moshi Vijijini, Antony Komu,  wote wa Chadema

“Historia ya zamani inatufunza matatizo yanayotokea katika jamii yanachangiwa na mambo yanayotendwa na baadhi ya watawala  ambayo yanaleta chuki.

“Na chuki siyo kitu kizuri kwa sababu inazidi kuwa kubwa kwenye mioyo ya watu hata kama wako kimya,”alisema na kuongeza:

“Hili limewahi kutokea enzi za mitume hata Nelson Mandela aliwekwa ndani na alipotoka dunia nzima iliamka hivyo tunaona kuna baadhi ya watu wanawekwa ndani bila sababu ya msingi, natoa wito kwa wenye mamlaka kuangalia suala hili.”

Mwenyekiti huyo alisema ni wakati wa watanzania wote kwa ujumla kupigia kelele suala hilo kwa vile  Mbunge ambaye ni mwakilishi wa wananchi, anazuiliwa kwa makosa yenye dhamana jambo la kukemewa.

“Tumekuja Arusha   kumuangalia Lema kwa sababu ni mwenzetu na tuna masikitiko na kama walifikiri wakimuweka Lema ndani wanamsimamisha au kumkomesha, wanamkomaza kisiasa.

“Anapata ujasiri wa aina Fulani kwa sababu  haelewi kwa nini yuko ndani, wangemkuta na malori matatu ya silaha sawa,” alisema.

Mbunge wa Bukoba Mjini alisema ameridhishwa na kupata matumaini na hali ya mbunge huyo kwa vile  ni yuleyule na ameongeza ujasiri wa kulisema lile analoamini.

Naye Mbunge wa Moshi Vijiji, Antony Komu,  alisema Lema ameomba wabunge wote bila kuangalia itikadi za vyama vyao wanapaswa kuwa makini wakati wa utungaji wa sheria.

Alisema   kutokana na baadhi ya upungufu wa sheria kuna watu wako gerezani kwa muda mrefu.

Alisema  katika gereza hilo asilimia kubwa wako gerezani kwa muda mrefu kutokana na upungufu wa sheria mbalimbali.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527