Kimenuka !! Wagonjwa Zaidi ya 20 Wanusurika Kufa Kwa Uzembe wa Madaktari Kituo Cha Afya Tinde ,Mbunge Acharuka,Angalia Picha


Wagonjwa 20 kati yao wanne wakiwa katika hali mbaya wamenusurika kifo baada ya kukosa huduma za matibabu kwa zaidi ya masaa tisa katika kituo cha afya cha Tinde kilichopo katika wilaya ya Shinyanga kutokana madaktari kutokwepo kituoni huku manesi wakiwa wamekaa tu kwenye wodi ya wazazi ambayo haikuwa na wagonjwa.


Kufuatia hali hiyo mbunge wa viti Maalum mkoa wa Shinyanga Mheshimiwa Azza Hilal aliyekuwa shambani kwake akiendelea na shughuli za kilimo, alilazimika kufika katika kituo hicho baada ya kupigiwa simu nyingi na wananchi waliofika kituoni hapo kupata huduma bila mafanikio tangu asubuhi.

Tukio hilo limetokea jana kati ya saa moja asubuhi na saa kumi jioni baada ya wagonjwa wanaodaiwa kuwa zaidi ya 20 kufika katika kituo hicho chenye jumla ya waganga watano kinachotoa huduma kwa zaidi ya kata 15 katika wilaya hiyo na wilaya jirani ya Nzega mkoani Tabora.

Inaelezwa kuwa waganga waliopo kituoni hapo ni wawili ambao ni Dr.Helena Kaunda na Dr. Zabela Sinzi,aliyetakiwa kuwa zamu ya asubuhi ni Zabela Sinzi aliyedaiwa kutofika kituoni kwa madai kuwa ni mgonjwa huku Dr.Helena Kaunda akitakiwa kuwa katika zamu ya mchana na kutokana na hali hiyo kituo kikawa hakina mganga na kusababisha usumbufu na kero kwa wagonjwa.

Mbali na mbunge huyo kufika katika kituo hicho,mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Kiomoni Kibamba alilazimika kufika baada ya kupigiwa simu na mbunge huyo aliyefika na kujionea hali halisi.
Mbunge huyo baada ya kufika katika kituo hicho majira ya saa tisa alasiri alikuta wagonjwa huku mmoja wa manesi (siyo wale wawili waliokuwa wodini) akiendelea kuwahudumia wagonjwa hao kwa kuwaandikia  na kwapa dawa wagonjwa na mkurugenzi alipofika alikuta zoezi la kutibu wagonjwa linaendelea ndipo wakaitisha kikao cha dharura na wafanyakazi wa kituo hicho

 Inaelezwa kuwa  Dr. Helena Kaunda alifika kituoni hapo majira ya saa tisa alasiri na kumkuta nesi huyo akiendelea kuwahudumia wagonjwa kwa kuwaandikia na kuwapa dawa.

Akizungumza katika kituo hicho majira ya saa kumi kasorobo, mbunge huyo alieleza kusikitishwa na kitendo cha watoa huduma kutojali wagonjwa tangu asubuhi hadi mchana bila sababu maalum.

“Nimepigiwa simu nyingi sana nilikuwa shambani,nimekuja hapa sijakuta mganga hata mmoja ,wakati kituo kina waganga watano,nimekwazika sana kituo hiki kinachohudumia watu wengi kikose mganga hata mmoja,kwa maelezo niliyopewa mmoja yuko likizo,mmoja anaumwa,hao watatu walikuwa wapi hadi wagonjwa wakose huduma tangu asubuhi?”,alihoji Mbunge huyo.

“Wagonjwa wamehudumiwa na mtu asiyestahili kuwaandikia,mkurugenzi naomba kukwambia kuwa nimekwazika,uzembe huu unasababisha sisi viongozi tunyoshewe vidole kwamba tunahusika,kwa hali hii nimepata majibu kwanini wananchi wetu hawataki kujiunga na bima ya afya kwa sababu ya kukosa huduma muhimu kwani hata walionipigia simu mmoja ana bima ya afya na hajapata huduma pamoja na kwamba alishalipia”,alieleza Hilal.

Aliongeza kuwa wakati wagonjwa wakisubiri wauguzi wasaidizi wawili walikuwa wanaendelea shughuli zao katika wodi ya wazazi ambayo hata hivyo hakikuwa na mgonjwa yeyote kitendo ambacho alidai kilimkwaza zaidi.

“Unawezaje kuwatazama watu wakikosa huduma kwa sababu tu eti wewe hukukabidhiwa na mganga,na huko ulikokaa hakuna mgonjwa yeyote,sasa inatosha,kila mtu awajibike kwa nafasi yake,kama kiongozi sikubali kituo hiki kukosa mganga hata mmoja kwani kinahudumia wagonjwa wengi”,aliongeza Hilali.

“Suala la gari pia limekuwa kero kubwa hapa,mganga na manesi wanaomba pesa kwa wananchi,mkurugenzi naomba ulifanyie kazi ujue nani anahusika…niseme tu kuwa katika kituo hiki hatuna mganga,na kuanzia huyu tuliye naye Dr.Helena Kaunda kuanzia sasa kwa kweli utafute mahali pa kumpeleka siyo hapa..Tinde sasa inatosha..ikiwezekana ondoka naye”,alieleza Hilal.

Alisema wananchi wanahitaji huduma wala siyo vyeti vya mtu na kwamba kauli pekee pia inachangia kuleta faraja kwa mgonjwa badala ya kutowahudumia wananchi.

“Nimeambiwa kuna mganga ameripoti hapa lakini hajawahi kuonekana,japo tunasikia anasema yeye ni msomi ana digrii hawezi kufanya kazi hapa,simjui wala sijawahi kuonana naye,lakini naomba majibu toka aripoti yuko wapi kwani hakutumwa kuja hapa kusaini kitabu na kuondoka,ametumwa kuja kusaidia wananchi ndiyo tunachokihitaji”,aliongeza mbunge huyo.

Aliwataka watumishi wa afya kubadilika na kuwajibika kwani hata kama hakuna dawa hakuna itajulikana kwani wagonjwa watasema kwamba kweli wameandikiwa dawa lakini hazipo badala ya kuwatazama tu bila kuwapa huduma.

“Mna matatizo ya kiutumishi kaeni na mkurugenzi mjadili,yamalizeni ya kwenu ya ndani hakuna sababu ya kuwaumiza wananchi wa kawaida,hawajui matatizo yenu,kama mnahitaji kuendelea kuwahudumia wananchi kaeni chini mjifikirie mara mbili,hatuwezi kufanya kazi kwa kusukumana,kuviziana”,alisema mbunge huyo.

Akizungumza wakati wa kikao cha dharura na wafanyakazi wa kituo hicho,mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Kiomoni Kibamba alimtaka mkuu wa kituo cha afya Tinde Hellena Kaunda na manesi wawili Ziada Samson na Happy Lameck kumpa maelezo kuhusu uzembe walionesha kabla hajachukua hatua zaidi dhidi yao.

Hata hivyo Kibamba alisema huduma ya gari ni bure kwa wagonjwa na kudai kuwa ni marufuku kwa mganga na manesi kuwatoza wagonjwa shilingi 40,000/= huku akiwataka wahudumu hao kupendana na kusaidiana pale wanapoona mwenzao kazidiwa.

“Lazima nichukue hatua,siko tayari kuwajibishwa kwa sababu ya uzembe wa mtu,baada ya kupata maelezo,nitakaa na bodi ya afya tujue tunachukua hatua gani,haiwezekani wananchi wateseke na sisi viongozi tupo,kuna malalamiko pia mnafika kazini saa moja asubuhi lakini mnaanza kuhudumia kuanzia saa nne ”,alisema Kibamba.

Naye mganga mkuu wa kituo cha Tinde Helena Kaunda alikiri kituo hicho kuwa na waganga wawili pekee kutokana na wawili kuwa wagonjwa na mmoja anashughulikia uhamisho na kwamba kilichotokea ni bahati mbaya kwani yeye hakuwa kituoni alipaswa kuingia mchana na aliyepaswa kuingia zamu ya asubuhi alikuwa anaumwa.

Nao wauguzi wasaidizi Ziada Samson na Happy Lameck waliodaiwa kuwa walikuwa kwenye wodi ya wazazi majira ya saa 4 asubuhi,walisema walikuwa wanaumwa ndiyo maana walishindwa kuwahudumia wagonjwa hao wanaodaiwa kuwa zaidi ya 20.

Mwenyekiti wa kijiji cha Jomu kata ya Tinde kilipo kituo hicho George Masele alizitaja baadhi ya changamoto zilizopo katika kituo hicho kuwa ni kauli mbaya za watoa huduma kwa wagonjwa,uhaba wa dawa,nyumba za wahudumu,wodi na jengo la upasuaji.

Angali picha hapa chini uone kilichojiri 



Baadhi ya wagonjwa waliokuwa wanasubiri huduma ya daktari katika jengo la OPD Tinde na wengine waliokaa hapo chini ya mti wakati mbunge Azza Hilal alipofika kituoni hapo.Aliyesimama katikati ni nesi aliyeanza kuhudumia wagonjwa ,ndiye alikuwa anaandika na kutoa dawa peke yake tangu saa nne asubuhi bila daktari,ambapo kuanzia saa moja asubuhi mpaka saa tisa alasiri ndipo Dr. Helena Kaunda alifika kituoni


Saa 10 jioni:Mbunge wa viti maalum mkoa wa Shinyanga (CCM) mheshimiwa Azza Hilal akizungumza katika kikao cha dharura na wafanyakazi wa kituo cha afya Tinde baada ya kupigiwa simu nyingi na wananchi wakilalamika kuhusu kukosekana kwa waganga katika kituo cha afya Tinde na kusababisha wagonjwa wakose huduma za afya kwa muda wa masaa 9.Mbunge huyo alikuwa shambani kwake akiendelea na shughuli za kilimo lakini akaamua kusitisha zoezi hilo kwenda kusikiliza kero za wananchi


Kulia ni mkurugenzi wa halmashauri ya Shinyanga Kiomoni Kibamba akiwa na mbunge Azza Hilal wakati wa kikao cha dharura na wafanyakazi wa kituo cha afya Tinde baada ya kupigiwa simu na mbunge huyo kuhusu uzembe uliosababisha kero kwa wananchi

Kulia ni mganga mkuu wa kituo cha afya Tinde Helena Kaunda akijitetea kwa mbunge Azza Hilal na mkurugenzi wa halamshauri ya wilaya ya Shinyanga Kiomoni Kibamba kwanini kituo hakikuwa na waganga tangu asubuhi mpaka saa tisa alasiri

Wafanyakazi wa kituo cha afya Tinde wakiwa katika kikao cha dharura

Wafanyakazi wa kituo cha afya Tinde wakiwa katika kikao cha dharura

Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Kiomoni Kibamba na mbunge Azza Hilal wakikagua daftari la mahudhurio katika kituo afya cha Tinde

Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Kiomoni Kibamba na mbunge Azza Hilal wakikagua daftari la mahudhurio katika kituo afya cha Tinde na kumhoji nesi wa kituo hicho Happy Lameck( kulia) ambaye jina lake lilionekana kuwa na makosa.Kushoto ni mwenyekiti wa kijiji cha Jomu kata ya Tinde kilipo kituo hicho George Masele akishuhudia kilichokuwa kinaendelea


Kulia ni Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Kiomoni Kibamba akizungumza katika kikao hicho

Kushoto ni mbunge wa viti maalum mheshimiwa Azza Hilal akizungumza katika kikao hicho cha dharura na kumuomba Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Kiomoni Kibamba kumuondoa mganga mkuu wa kituo hicho kutokana na uzembe ambao amekuwa akiuonesha mara kwa mara kituoni hapo na kusababisha viongozi wa serikali kuonekana hawafai kwa wananchi

Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Kiomoni Kibamba akiwasisitiza watoa huduma hao kupendana na kusaidiana katika kazi huku akiahidi kuchukua hatua kwa mganga mkuu wa kituo hicho Dr. Helena Kaunda kwa mujibu wa taratibu za kazi

Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Kiomoni Kibamba(katikati) akizungumza katika kikao hicho,kulia ni mganga mkuu wa kituo cha afya Tinde Helena Kaunda,kushoto ni mheshimiwa Azza Hilal

Kikao kinaendelea kulia ni kaimu mganga mkuu wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Dr.Mikael Kalomwa Jidamabi akisikiliza kwa umakini maelezo ya Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Kiomoni Kibamba

Ziada Samson mmoja wauguzi wanaodaiwa kukaa wodini bila mgonjwa yeyote huku wagonjwa wakihitaji huduma,alisema alishindwa kuhudumia wagonjwa kwa sababu alikuwa anaumwa

Happy Lameck,nesi mwingine anayedaiwa kuwa katika wodi ya wazazi akizungumza na waandishi wa habari ambapo alisema hakuhudumia wagonjwa kwa sababu alikuwa anaumwa

Mganga mkuu wa kituo cha afya Tinde Dr. Helena Kaunda akizungumza na waandishi wa habari ambapo alisema wakati wagonjwa wanakosa huduma hakuwa kituoni kwa haikuwa zamu yake na kwamba kituo hicho kina waganga wawili tu hivi sasa baada ya wawili kuugua na mmoja akiwa katika taratibu za kutafuta uhamisho

Mbunge Azza Hilal akiwa ndani ya wodi ya wazazi isiyo na wagonjwa ,ambayo walikuwa wamekaa manesi wawili huku wagonjwa wakihangaika nje

Mbunge akiwa wodini na viongozi wa kijiji cha Jomu,kaimu mganga mkuu wa halmashauri hiyo

Wodi ya wazazi ambamo walikuwa wamekaa manesi hao

Wodi ya wazazi ikiwa haina wagonjwa

Mheshimiwa Azza Hilal akiwa wodini

Mheshimiwa Azza Hilal akiteta jambo na mwenyekiti wa kijiji cha Jomu George Masele

Moja ya majengo katika kituo cha afya cha Tinde

Gari la wagonjwa katika kituo cha afya Tinde

Jengo katika kituo cha afya Tinde

Jengo katika kituo cha afya Tinde

Jengo katika kituo cha afya Tinde

Bango likionesha muda wa kuona wagonjwa

Jengo katika kituo cha afya Tinde
Picha zote na Kadama Malunde-Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post