EZEKIAH WENJE AFUNGA USHAHIDI AKIWA PEKE YAKE KESI YA UBUNGE




Upande wa madai katika kesi ya kupinga matokeo ya ubunge wa Nyamagana jana ulifunga ushahidi baada ya Mahakama Kuu kukataa ombi la kutumia fomu namba 21B kwa ajili ya mashahidi wengine.


Baada ya kufunga ushahidi katika kesi hiyo namba 5/2015, mbunge wa zamani wa jimbo hilo (Chadema), Ezekiah Wenje dhidi ya Stanslaus Mabula (CCM), upande wa utetezi leo unatarajiwa kuwasilisha hoja iwapo nao unafunga ushahidi au utaita mashahidi mahakamani.


Hatua hiyo imekuja jana baada ya Jaji Kakusilo Sambo kukubaliana na pingamizi lililowekwa na upande wa wajibu maombi wakipinga mleta maombi kutumia fomu hizo katika ushahidi wake.


Katika pingamizi la mawakili wa utetezi, Vicent Tangoh anayemuwakilisha Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Constantine Mutalemwa anayemuwakilisha Mabula, walidai mdai hakutoa fomu hizo kwa utetezi ili kuzihakiki kwa muda mwafaka kama alivyoagizwa na Mahakama, hivyo hazistahili kutumika mahakamani.


Upande wa utetezi ulidai licha ya kutowasilisha fomu hizo kwa muda mwafaka, pia mlalamikaji aliziwasilisha kwa kutumia vifungu tofauti bila kuieleza Mahakama sababu za msingi za kutaka aruhusiwe kuzitumia kama kielelezo.


“Fomu hizi ndizo kiini cha maombi haya na mdai alipewa siku 10 kuzikabidhi kwa upande wa utetezi ili kuzihakiki na kuandaa hoja za majibu, hakufanya hivyo na kushindwa kutoa sababu za msingi za kutofanya hivyo,” alidai wakili Tangoh.


Baada ya Mahakama kukubaliana na pingamizi hilo, wakili wa Wenje, Deya Outa aliomba kufunga ushahidi kwani hawataweza kuita shahidi mwingine kutokana na ushahidi wao wote kutegemea fomu zilizokataliwa.


Jaji Sambo alikubaliana na ombi hilo baada ya upande wa utetezi kutokuwa na pingamizi na kuahirisha kesi hiyo hadi leo mawakili hao wa utetezi watakapowasilisha hoja zao, iwapo wanafunga ushahidi au kuita mashahidi kupinga ushahidi wa Wenje ambaye ni shahidi pekee wa upande wa mlalamikaji.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post