DC AMSWEKA RUMANDE MWENYEKITI WA KIJIJI KWA KUWAFUKUZA MAOFISA ARDHI




Mwenyekiti wa Kijiji cha Munge kilichopo kata ya Donyomurwa, wilaya ya Siha mkoani Kilimanjaro, Peter Laiza, ameswekwa rumande kwa amri ya Mkuu wa Wilaya hiyo, Dk Charles Mlingwa, kutokana na kuwafukuza Maofisa Ardhi waliokuwa katika mpango wa kutatua mgogoro wa ardhi.


Mgogoro huo wa ardhi unadaiwa kukihusu kijiji cha Munge kinachoongozwa na Mwenyekiti huyo pamoja na eneo la Kilelepori linalotumiwa na Chuo cha Taaluma ya Polisi (MPA).


Katika kuupatia ufumbuzi mgogoro huo, Mkuu wa Wilaya aliwatuma Maofisa Ardhi ili upimaji ufanyike katika baadhi ya maeneo ya wananchi.


Hata hivyo, inadaiwa kwamba Dk Mlingwa alichukua hatua hiyo bila kutoa taarifa kwa uongozi wa kijiji, hali iliyomlazimu mwenyekiti huyo kuwakataza maofisa hao kufanya kazi hiyo kijijini kwake.


Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro, Wilbrod Mutafungwa, alithibitisha kukamatwa na kuwekwa ndani kwa mwenyekiti huyo, kwa kile alichoeleza ni kutokana na amri ya Mkuu wa Wilaya ya Siha, Dk Mlingwa.


Hata hivyo, Diwani wa Kata ya Donyomurwa, Luite Ndoss, alisema hakuwa na taarifa zozote za kushikiliwa kwa kiongozi huyo, bali taarifa hizo alizipata baada ya kufika katika kituo cha Polisi akiwa anafuatilia mambo yake binafsi.


Kutokana na mgogoro huo, Mkuu wa Wilaya aliitisha kikao cha Serikali ya Kijiji Machi 30 lakini mwenyekiti huyo hakuweza kuhudhuria kwa sababu shauri la mgogoro huo liko katika Mahakama ya Ardhi. Diwani Ndoss pia hakuhudhuria kikao hicho.


“Kitendo cha Mkuu wa Wilaya kutoa amri ya Mwenyekiti wa Kijiji cha Munge kuwekwa ndani ni jambo la uonevu, na kitendo hicho kinazidi kuongeza mgogoro kati ya wananchi na Mkuu wa Wilaya,” alidai Ndoss.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post