AUAWA KWA KUCHOMWA KISU AKIAMUA MGOGORO WA MAPENZI




Mtu mmoja amefariki dunia, huku mwingine akijeruhiwa baada ya kuchomwa visu wakati wa ugomvi uliotokana na wivu wa mapenzi wilayani Ilemela mkoani Mwanza.


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Justus Kamugisha alimtaja aliyeuawa kuwa ni Makororo Kitota (26) ambaye ni mkazi wa Mtaa wa Iloganzala, alichomwa kisu shingoni na kifuani na kupoteza maisha palepale.


Alisema tukio hilo lilitokea Machi 30, mwaka huu saa nne usiku katika kilabu ya pombe za kienyeji.


Kamugisha alisema mtuhumiwa aliyefanya tukio hilo alikuwa na ugonvi wa muda mrefu na Kitota akimdhania kuwa na uhusiano wa kimapenzi na mkewe ambaye pia alikuwapo kilabuni hapo wakati wa tukio hilo.


Kwa mujibu wa kamanda huyo, wanandoa hao walikuwa wametengana tangu Agosti 2015 kwa sababu hiyo hiyo kutokana na usaliti katika uhusiano wa kimapenzi.


Aliyejeruhiwa katika tukio hilo ni Nchama Wanda (33), mkazi wa Sabasaba wilayani humo aliyechomwa kisu tumboni na utumbo kutoka nje alipojaribu kuwaamulia wakati wakipigana.


Kamugisha alisema majeruhi huyo amelazwa katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando kwa matibabu zaidi na kwamba, hali yake siyo nzuri.


Alisema mke wa mtuhumiwa wa mauaji hayo anashikiliwa na polisi baada ya mtuhumiwa na mmiliki wa kilabu hiyo kukimbia kusikojulikana.


Kamanda huyo alisema jeshi hilo linaendelea kuwatafuta watu hao ili kuwafikishwa kwenye vyombo vya sheria.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527