Basi Lagongana na Hiace Huko Kigoma,Watu Wawili Wafariki Dunia



Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani Kigoma,SACP,Frednand Mtui


Watu wawili wamefariki dunia na wengine wawili kujeruhiwa katika ajali iliyohusisha gari aina ya Toyota Hiace lenye namba za  usajili T.502 BKY na gari lenye namba za usajili T.321 BHC Bus Scania kampuni ya Ncheye Bus Service Mwanza katika Kijiji cha Bugaga kata ya Bugaga tarafa ya Heru Chini wilayani Kasulu mkoani Kigoma.



Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani Kigoma,SACP,Frednand Mtui aliwataja waliofariki katika ajali hiyo kuwa  ni,Essau Johnson (20) Mkazi wa Kijiji cha Bugaga na Mwanamke mmoja ambaye jina lake halikufahamika.


Tukio hilo limetokea tarehe Aprili 17,2016 majira ya saa 11 jioni huko katika kijiji cha Bugaga Wilayani Kasulu Mkoani Kigoma .


Mtui alisema kuna majeruhi wawili waliojeruhiwa katika ajali hiyo na chanzo cha ajali hiyo ni mwendokasi wa dereva wa Hiace uliopelekea kushindwa kulimudu gari lake kisha kuligonga basi hilo walipokuwa wakipishana darajani.



"Baada ya ajali hiyo kutokea dereva aliyefahamika kwa jina la,Sologo Nkeshimana Mkazi wa Kijiji cha Mwandiga Wilaya ya Kigoma vijijini alikimbia baada ya kusababisha ajali hiyo",alisema Mtui.


Alisema majeruhi wote wanaendelea kupatiwa matibabu katika Hospitali ya Wilaya ya Kasulu na hali zao zinaendelea vizuri na dereva alieye sababisha ajali hiyo anaendelea kutafutwa ili aweze kufikishwa mahakamani.


Jeshi la polisi mkoani humo linawaomba madereva wote kutii sheria na kufuata sheria za usalama barabarani ili kupunguza vifo na majeruhi vinavyotokana na uzembe wa madereva wazembe.
Na Rhoda Ezekiel -Malunde1 blog Kigoma

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post