MWANAFUNZI WA CHUO HUKO DODOMA AMUUA MWENZAKE WAKIGOMBANIA CHAJA YA SIMU





Watu wawili wamefariki dunia mkoani Dodoma katika matukio mawili tofauti likiwemo la mwanafunzi wa chuo cha serikali za mitaa Hombolo, Basil Msabila (24) kuuawa kwa kupigwa na chuma kichwani na mwenzake aitwaye Charles Makele (19) kwenye ugomvi wa kugombea chaja ya simu.

Akizungumza na waandishi wa habari, kamanda wa polisi Mkoa wa Dodoma, Lazaro Mambosasa amesema kuwa tukio hilo lilitokea Machi 6 mwaka huu katika chuo cha serikali za mitaa kilichopo Hombolo katika Manispaa ya Dodoma.

Amesema uchunguzi wa awali unaonesha kuwa chanzo cha tukio hilo ni ugomvi wa kugombania chaja ya simu ambayo ni mali ya marehemu katika chumba cha bweni ambapo wanaishi wanafunzi wanne.

Katika tukio la pili mtu mmoja mwanaume ambaye hakufahamika jina lake mara moja aliuawa na watu wenye hasira katika eneo la kisasa lililopo katika Manispaa ya Dodoma baada ya kukutwa akivunja dirisha la mtu.

Aidha ametoa wito kwa wananchi wa mkoa wa Dodoma kutojichukulia sheria mkononi na kutofanya mauaji ya kikatili dhidi ya watu kwa tuhuma nyepesi kwa kisingizio cha watu wenye hasira kali .

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527