Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

POLISI SHINYANGA WAANDAMANA BADALA YA CHADEMA KUPINGA MATOKEO YA UCHAGUZI MKUU 2015 YALIYOTANGAZWA NA TUME YA UCHAGUZI




Gari la maji ya kuwasha likiwa mtaani-Picha kutoka Maktaba ya Malunde1 blog

Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) wilaya ya Shinyanga mjini kimesema kimefanikiwa kufanya maandamano yao ya amani kupinga matokeo ya uchaguzi mkuu 2015  yaliyotangazwa na tume ya taifa ya uchaguzi kupitia askari wa jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga.


Akizungumza na Malunde1 blog mapema leo katibu wa Chadema wilaya ya Shinyanga mjini George Kitalama amesema wamefanikiwa kufanya maandamano yao kupitia jeshi la polisi akidai kuwa polisi wameandamana badala ya Chadema wakiwa na magari yao mtaani.




Kitalama amesema walipanga kufanya maandamano mji mzima wa Shinyanga lakini polisi ndiyo wamejitokeza kufanya maandamano kwa magari yao kila mtaa  katika wilaya ya Shinyanga.

“Chadema leo tumefanya maandamano ya aina yake,polisi wametusaidia kuandamana na magari yao mtaani kwa niaba yetu,hivyo maandamano yetu yamefanikiwa na watanzania wamepata ujumbe tuliotaka uwafikie kuwa tunapinga matokeo ya uchaguzi mkuu 2015 yaliyotangazwa na tume ya taifa ya uchaguzi”,amefafanua Kitalama.

Amesema tangu Novemba 02,2015 hadi Novemba 03,2015 misururu ya magari ya polisi yakiwemo ya maji ya kuwasha yakiwa na askari polisi yamekuwa yakiranda randa mtaani hivyo hiyo ni ishara tosha kuwa polisi wanaandamana badala ya Chadema.

Hata hivyo kitendo cha Chadema kusitisha maandamano yao katika wilaya ya Shinyanga kumepongezwa na baadhi ya wananchi kwa madai kuwa kungesababisha uvunjifu wa amani huku wakishauri kuwa kama kweli Chadema hajaridhishwa na matokeo hayo basi wasiruhusu hata wabunge wao kuapishwa.

Kwa upande wao baadhi ya wakazi wa Shinyanga wamesema ni vyema serikali ingewaruhusu wafuasi wa Chadema  waandamane ili kueleza hisia zao juu ya matokeo ya uchaguzi mkuu uliopita kwani ni maandamano ya amani.

Kusitishwa kwa maandamano ya Chadema kumekuja siku moja tu baada ya jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga kuzuia maandamano na mikutano yote katika kipindi hiki hadi pale wabunge na rais mteule wa jamhuri ya muungano wa Tanzania atakapoapishwa ili kuimarisha ulinzi na usalama katika nchi kwa kuepuka vitendo vyote vinavyoweza kuleta uvunjifu wa amani.

Na Kadama Malunde-Malunde1 blog
SOMA HAPA TAARIFA YA JESHI LA POLISI KUZUIA MAANDAMANO YA CHADEMA

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com