WANANCHI WACHOMA MOTO KITUO CHA POLISI HUKO MOROGORO KISA MAUAJI YANAYOTOKANA NA MAPENZI


Kundi la watu zaidi ya 100 wakiwa na silaha mbalimbali za jadi ikiwemo mapanga, mawe na marungu wamevamia kituo kidogo cha polisi cha Mbingu, kilichopo tarafa ya Mngeta wilayani Kilombero, mkoani Morogoro kukipiga mawe na kukichoma kwa moto, wakishinikiza kukabidhiwa ili wamuue mtuhumiwa waliyemfikisha polisi muda mchache kabla, aliyekuwa akituhumiwa kumuua mkewe kutokana na wivu wa kimapenzi.


Tukio hilo lililothibitishwa na polisi, limetokea kituo kidogo cha polisi cha Mbingu kilichopo umbali wa takribani kilometa 60 kutoka mji mdogo wa Ifakara, ikiwa ni saa chache baada ya mtuhumiwa Bashiri Ernest Kadugula kufikishwa kituoni hapo akikabiliwa na tuhuma za kumuua mkewe, Veronica Chambula kwa kumkata kata kwa panga.

Tukio hilo limetokea  baada ya kutokea tofauti baina yao, na mke kuamua kukimbilia kwa wazazi wake, lakini mumewe alidhani alikuwa amekwenda kwa mwanaume mwingine.

Kamanda wa polisi mkoa wa Morogoro Leonard Paulo amesema polisi walifanikiwa kumtorosha mtuhumiwa Kaduguda aliyekuwa akitafutwa, sambamba na baadhi ya silaha, kabla ya wananchi hao kukipiga mawe na kukiteketeza kwa moto kituo hicho cha polisi.

Pia walisababisha pikipiki tano zikiwemo mbili za askari polisi, PC Wilson na PC Isaya kuteketea, sambamba na kuvunja mlango wa ofisi ya kijiji cha mpofu na kuchoma moto nyaraka mbalimbali zilizokuwemo, na tayari watuhumiwa 11 wametiwa mbaroni kuhusiana na tukio hilo.

Kufuatia tukio hilo, wananchi wa mkoa wa Morogoro wamelaani matukio ya wananchi kuvamia vituo vya polisi na ofisi nyingine za serikali, kuzichoma moto na hata kusababisha hasara mbalimbali.

Via>>>ITV

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post